Adverts

Showing posts with label Usalama. Show all posts
Showing posts with label Usalama. Show all posts

Tuesday, October 4, 2016

Polisi Aliyerekodiwa Akipokea Rushwa Kuchukuliwa Hatua

 
Jeshi  la Polisi visiwani Zanzibar, limesema litamchukulia hatua za kinidhamu ofisa wake mwenyewe cheo cha Sajenti ambaye alionekana hivi karibuni akipokea rushwa kutoka kwa raia wa kigeni.

Hatua hiyo, imekuja baada ya picha za video kusambaa katika mitandao ya kijamii, zinazomwonyesha askari huyo akipokea fedha ambazo hadi sasa hazijajulikana kiwango chake kutoka kwa raia huyo wa kigeni, ambaye alikuwa na kosa la kutofunga mkanda.

Katika video hiyo, raia huyo anaokana kutoa fedha na kumkabidhi askari huyo huku akiahidi kumsaidia ili asikamatwe mbele ya safari.

Tukio hilo lilitokea eneo la Mkokotoni Mkoa wa Kaskazini Unguja, ingawa askari huyo alitaja eneo la Mahonda akionyesha nia ovu ya kutenda kosa hilo bila kujijua kama anachukuliwa video.

Kamishna wa Jeshi la Polisi Zanzibar, Hamdani Omar Makame alisema jeshi hilo linampongeza raia huyo wa kigeni kwa kutoa taarifa hiyo.

“Jeshi la polisi linachukua nafasi hii kulaani kosa hili, licha ya kua ni kosa la jinai linalifedhehesha jeshi na kulitia doa kutokana na dhamana kubwa lililokabidhiwa,” alisema.

Alisema kwa mujibu  wa taratibu za jeshi hilo, tayari limeanza uchunguzi mara moja na kwamba litachukua hatua zinazostahili.

Kutokana na hali hiyo, Kamishina Hamdani amewataka wamiliki wa makampuni ya simu za mikononi kufufua mfumo wa upigaji simu kutumia namba za dharura ambazo ni 111 na 112 ili kuwarahisishia wananchi kutoa taarifa.

Tazama Video ya tukio hapa chini.

Sunday, October 2, 2016

Unyama Unyama: Watafiti Watatu toka Chuo cha Selian Wauawa na Wananchi Kwa Kuchomwa Moto Wakidhaniwa ni Wanyonya Damu

Yowe ya kuvamiwa na wanyonya damu , iliyopigwa na wanawake waliokuwa wakichimba chumvi katika Kijiji cha Iringa-Mvumi wilayani Chamwino, Mkoa wa Dodoma ndiyo iliyosababisha kuuawa kwa watafiti wa Chuo cha Utafiti wa Udongo na Maendeleo ya Ardhi cha Selian mkoani Arusha.

Watafiti hao waliuawa juzi kwa kukatwa katwa mapanga na minde, kisha kuchomwa moto. Gari la Serikali aina ya Toyota Hillux, pia lilichomwa moto.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba wanawashikilia watu kadhaa akiwamo mwenyekiti wa kijiji.

Alisema mwenyekiti wa kitongoji alipigiwa simu na mmoja wa wanawake waliokuwa eneo la tukio kwamba kuna wanyonya damu wamevamia kijiji.

Mambosasa alisema kwa kuwa mwenyekiti huyo alikuwa mbali, alimpigia simu mwenyekiti wa kijiji aende eneo la tukio kujua kilichotokea. Alisema mwenyekiti wa kijiji alipofika hakuamini maelezo ya watafiti hao na kuanza kuwashambulia.

Mambosasa alisema mtu mwingine alikwenda kijijini na kumueleza mchungaji wa kanisa kuhusu kijiji kuvamiwa na nyonya damu, naye akatagaza kwenye kipaza sauti kwamba kijiji kimevamia na watu hao.

Alisema wanakijiji walijitokeza kwenda eneo la tukio na kuwashambulia watafiti hao hadi kufa.

Mkuu wa Mkoa, Jordan Rugimbana alisema baada ya kutembelea eneo la tukio, ameamua kuwasimamisha kazi kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya Chamwino na ofisa utumishi wa wilaya hiyo kwa madai ya kutosambaza barua za kuwatambulisha watafiti hao katika maeneo waliyokwenda kufanya kazi.

Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Simon Kawea alisema taarifa alizozipata kutoka kwa diwani wa kata ya Iringa-Mvumi, watafiti hao walipofika katika eneo la Makamwa walikutana na watu na kuwauliza kilipo kijiji cha Iringa-Mvumi.

Kawea alisema watafiti hao walipofika eneo walilotaka kufanya utafiti walipigiwa yowe kwamba ni wanyonya damu.

Alisema baada ya kelele zile wanakijiji waliokuwa katika mkutano walisikia na kutoka na mapanga na silaha za jadi kisha kuwavamia watafiti hao na kuwashambulia kwa silaha hizo.

“Hata walipoonyesha vielelezo wao si wezi bali ni watafiti waliopewa kibali na halmashauri ya Chamwino na vielelezo vingine, wanakijiji walikataa na kuendelea kuwapiga,” alisema.

Alisema watendaji wa kijiji hicho na diwani wa kata hiyo, Robert Chikole waliwasihi wanakijiji kuwaacha watafiti hao lakini walizidiwa nguvu na wananchi.

Aliongeza: “Hata polisi walifika muda mfupi, walikuta wameumizwa vibaya wakarusha risasi juu lakini walizidiwa nguvu na kukaa pembeni. Kwa kweli wamekufa katika tukio la kinyama,” alisema.

Alisema watafiti hao walikwenda katika ofisi za Wilaya ya Chamwino na kupata kibali kabla ya kwenda kijijini hapo kwa ajili ya kufanya utafiti wa udongo.

Alisema diwani, mtendaji na mwenyekiti wa kijiji wanashikiliwa na polisi kuhusiana na tukio hilo.

Habari kutoka kijijini hapo zinasema wanakijiji wamekimbia makazi yao kutokana na msako wa polisi kwenye eneo hilo.

Majonzi yatawala Arusha
Mauaji ya hayo yameibua simanzi katika taasisi ya Selian na familia zao, ikiwamo ya mkurugenzi wa taasisi hiyo, Dk January Mfuru ambaye mtoto wake pia ameuawa.

Mtoto huyo, Faraji Mafuru amehitimu Chuo cha Mipango Dodoma hivi karibuni na alikuwa katika mazoezi kwa vitendo.

Mratibu wa utafiti katika kituo hicho, Dk Charles Lyamchai alisema tukio hilo limetokea wakati timu ya watafiti wa kituo hicho ikiwa mkoani Dodoma kutekeleza mradi wa kukusanya sampuli za udongo kwa ajili ya kuziingiza kwenye kanzidata ya Taifa.

“Hawa walikuwa kwenye mradi maalumu ambao umeanza mwaka 2014 na wapo wengine watafiti ambao wamesambaa kwenda mkoani Dodoma kwa kazi hii,” alisema.

Aliwataja wengine waliouawa kuwa ni dereva Nicas Magazine na Mtafiti wa maabara ya udongo, Teddy Lumanga.

“Wapo watumishi 10 huko kutoka hapa kituoni, waliokwenda kutekeleza mradi wa kutambua kiwango cha rutuba kwenye udongo nchini ambao tumeshaukamilisha kwenye wilaya zote za mikoa ya Kanda ya Kaskazini na Katavi na wilaya ya Kondoa, hili ni jambo la kushtua sana,” alisema.

Alisema watafiti hao walikuwa katika wiki ya pili na hawakuwa wamepata matatizo yeyote tangu wafike Dodoma, baada ya tukio hilo kiongozi wa msafara aliwasiliana na kituo.

Dk Lyamchai alisema kabla ya  kwenda huwa wanatoa taarifa kwa kuandika barua kwenye wilaya husika, pia maeneo ya vijijini huwa wanaambatana na mabwana shamba.

“Watafiti wetu hawana mahusiano yoyote na masuala ya damu, walikuwa kwenye kazi zao na walitoa taarifa hadi ofisi ya kata ila hatujui ni kwa nini tukio hili limejitokeza,” alisema.

Mtafiti mwandamizi wa kituo hicho, Dk Lameck Makoye alisema hawajawahi kukutana na changamoto kubwa kama hiyo hasa maeneo ambayo huwa na historia ya wenyeji wasiopenda wageni.

Alisema Dk Mafuru na watafiti wengine waliondoka jana kwendas Dodoma kuungana na watafiti wengine kutoka Kituo cha Hombolo na Makutupola kwenda eneo la tukio.

Selian ni miongoni mwa vituo maarufu katika Ukanda wa Afrika ya Mashariki na Kati kwa kufanya tafiti za mazao katika maeneo yenye ukame nchini.

Thursday, September 1, 2016

Rais Dkt. Magufuli Awapongeza JWTZ Kwa Kutimiza Miaka 52 Tangu Kuanzishwa Kwake

Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuwaunga mkono na kuwatumia wahandisi wa ndani wenye ujuzi mbalimbali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa viwanda, reli, barabara na miundombinu mingine.

Hayo yamesema na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, alipokuwa akifungua Mkutano wa 14 wa mwaka wa wahandisi unaofanyika kwa siku mbili kuanzia leo tarehe 01 Septemba, 2016 katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.
 
Dkt. Magufuli amesema atafurahi kuona miradi inayohusisha kazi za kihandisi na hasa wakati huu ambapo nchi inaelekea katika uchumi wa viwanda inatekelezwa kwa kutumia wahandisi wa ndani na hivyo amewataka kujipanga sawasawa ili kukabiliana na changamoto hiyo.

"Nyinyi wahandisi mkiamua nchi hii iende kwenye uchumi wa kati tutafika, mkiamua nchi hii iende kwenye uchumi wa viwanda tutafika, na msipoamua hatutafika. 
 
"Sasa hivi kuna ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (Standard gauge) kwani nyinyi mnashindwa kujenga?" Amehoji Rais Magufuli huku akisisitiza kuwa Serikali yake ipo tayari kuwaunga mkono pale watakapohitaji msaada.
 
Hata hivyo Dkt. Magufuli amewakumbusha umuhimu wa kufanya kazi kwa ubora, ushirikiano na upendo miongoni mwao huku akielezea kusikitishwa kwake na baadhi ya wahandisi ambao wamekuwa wakifanya vitendo vya ukiukwaji wa maadili ikiwemo kushirikiana na wakandarasi na wazabuni kuzidisha viwango vya makadirio ya gharama za miradi na manunuzi ya Serikali ili kujipatia fedha isivyo halali na kupitisha miradi iliyojenga chini ya viwango.
 
Rais Magufuli ameongeza kuwa Serikali yake itaendelea kuchukua hatua kali dhidi ya wote wanaotumia vibaya fedha za umma na amesisitiza kuwa hatua zaidi za kuhakikisha kunakuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha za Serikali zitachukuliwa.
 
"Kuna watu wanasema mzunguko wa pesa umepungua na hali imekuwa ngumu, hizo pesa zilizokuwa zinachezewa huko mitaani zilikuwa pesa za Serikali, mimi nataka pesa ziende kwenye miradi ya maendeleo na ndio maana bajeti ya maendeleo tumeongeza kutoka asilimia 26 hadi asilimia 40" Amesisitiza Rais Magufuli.
 
Katika tukio jingine, Rais Magufuli amewatembelea Askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Kikosi cha 603 (Air Wing) kilichopo Ukonga Jijini Dar es Salaam na kuwapongeza kwa kuadhimisha miaka 52 ya tangu kuanzishwa kwa Jeshi hilo. 
 
Katika kuadhimisha miaka 52 ya JWTZ Askari wa Jeshi hilo wamefanya usafi katika maeneo mbalimbali.
 
Pamoja na pongezi hizo Rais Magufuli amekagua baadhi ya ndege zinazotumiwa na Jeshi hilo na amewahakikishia Wanajeshi kuwa Serikali yake itaendelea kuliimarisha Jeshi hilo kwa vifaa na maslai ya Askari ili kuendelea kuwa na Jeshi bora, la kisasa na lililo tayari kuilinda nchi wakati wote. 
 
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es Salaam
01 Septemba, 2016

Wednesday, August 31, 2016

Waziri Mwinyi: Mipaka ya Tanzania iko Salama.

 
Na: Lilian Lundo- Maelezo
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amewahakikishia watanzania kwamba mipaka ya Tanzania ni salama.

Mhe. Dkt. Mwinyi ameyasema hayo katika kipindi cha Tunatekeleza kinachorushwa na Televisheni ya Taifa (TBC) alipokuwa akieleza mikakati ya wizara hiyo katika kuhakikisha mipaka ya Tanzania iko salama.

“Nchi iko salama, mipaka ya nchi iko shwari, ziko changamoto chache za nchi zinazotuzunguka kuwepo katika machafuko mfano Burundi hivyo wananchi wake kukimbilia Tanzania,” alifafanua Mhe. Dkt. Mwinyi.

Amesema Tanzania sio kisiwa, imejiunga na jumuiya mbali mbali kama Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Umoja wa Afrika na Jumuiya ya Umoja wa Mataifa hivyo kupitia Jumuiya hizo Tanzania hupata maelekezo ya kuwapokea wakimbizi kutoka nchi zenye machafuko.

Hata hivyo Mhe. Dkt. Mwinyi amesema kuwa Wizara yake kwa kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi inahakikisha wakimbizi wanaoingia nchini wanafuata utaratibu unaotakiwa bila kuvunja sheria za nchi.

Pia ameeleza kuwa Tanzania inaendelea na mazungumzo ya amani na nchi ya Malawi juu ya mgogoro wa umiliki wa Ziwa Nyasa baina ya nchi hizo mbili ili kupata ufumbuzi wa amani, ambapo mazungumzo hayo ya yanaongozwa na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Benjamin William Mkapa.

Aidha, Mhe. Dkt. Mwinyi amesema kuwa kutokana na Wizara hiyo kufanya vizuri katika Ulinzi na Amani ya Nchi, Jumuiya ya Umoja wa Afrika na Jumuiya ya Umoja wa Mataifa imeiomba nchi ya Tanzania kutoa Ulinzi wa  Amani kwa nchi za Sudani, Kongo na Lebanoni kutokana na machuko yanayoendelea katika nchi hizo.

Vile vile ameeleza kuwa, ushiriki wa Jeshi la Tanzania katika nchi zenye machafuko kunaisaidia Jeshi hilo kupata mafunzo ya kivita kutokana na Tanzania kuwa ni nchi ya amani hivyo kufanya baadhi ya wanajeshi kutoshiriki mafunzo ya uhalisia ya kivita tangu wanapoajiriwa mpaka kustaafu.

Ndege za Kivita Kutawala Anga la Dar Septemba 1

 
Septemba mosi mwaka huu inataraji kuingia katika histori ya Tanzania kutokana na matukio ambayo yanataraji kufanyika siku hiyo, matukio hayo ni pamoja na sherehe za miaka 52 ya Jeshi la Wananchi la Tanzania (JWTZ), maandamano ambayo yamepangwa kufanywa ya UKUTA na tukio la kupatwa kwa jua.

Akizungumza na Waandishi wa Habari wakati alipokutana na Maafisa wa Jeshi la JWTZ Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alisema JWTZ inapotimiza miaka 52 ni fahari kubwa hivyo tunapaswa kuwapongeza kwa kudumisha amani na mshikamano.

Alisema Jeshi hilo limejipanga kurusha angani ndege zake za kivita katika anga la Dar es Salaam, Septemba 1 mwaka huu, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 52 ya kuanzishwa kwake.

Makonda aliwataka wananchi kutokuwa na hofu wanaposikia ngurumo za ndege hizo bali wafurahie kwani ni ndege zao.

“Mnaposikia milio ya ndege zetu mbalimbali, mfurahie kwa sababu hizo ni ndege za wananchi. Usisikie muungurumo ukashtuka. Hakuna jambo lolote lile zaidi ya kuonesha vifaa vyetu na jinsi ambavyo wanajeshi wetu kwa miaka 52 wamaeendelea kuwa imara na vifaa vizuri,” alisema Makonda.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa waliwataka wananchi waliojipanga katika vikundi mbalimbali kuripoti kwa wakuu wao wa wilaya kujiandikisha ili waweze kushiriki pamoja na Jeshi hilo katika zoezi la usafi jijini humo.

Aliwataka wakazi wa mkoa huo pia kujitokeza kuchangia damu katika vituo mbalimbali ambavyo vimeanishwa ili kuunga mkono juhudi za uchangiaji damu zitakazofanywa na wanajeshi wa JWTZ.

“Hii ni sehemu ya amani, tufanye usafi kwa amani. Tujitolee damu zetu kwa amani na mwisho wa siku tuwaenzi na kuwapongeza wanajeshi wetu kwa kazi kubwa wanayoifanya,” Makonda alieleza.

Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa aliendelea kutoa onyo kwa watu watakaotaka kufanya maandamano yaliyopigwa marufuku ya oparesheni UKUTA akiwataka kutii sheria.

“Mimi ninavyojua UKUTA ni kuwa mtu amefika mwisho wa kufikiri sasa kama watakuwa wamefika mwisho wa kufikiria basi sisi tutawasaidia … watu wapo wanapanga kufanya mambo ya kusaidia jamii wao wanapanga maandamano nawashauri wananchi waungane na Polisi,” alisema Makonda.

Tuesday, August 30, 2016

Tamko La Mtandao Wa Watetezi Wa Haki Za Binadamu Dhidi Ya Mauaji Ya Askari Wa Jeshi La Polisi

Mtandao wa Watetezi wa Waki za Binadamu (THRDC) kwa niaba ya wanachama wake tunalani vikali maujai ya askari wa jeshi la polisi huku tukisisitiza kwamba askari wa jeshi la polisi wanaofanya kazi katika misingi na sheria ni watetezi wa haki za binadamu kama walivyo watetezi wengine. 

Kutokana na taarifa rasmi ya jeshi la polisi ni kwamba mnamo tarehe 23/08/2016 saa moja usiku maeneo ya Mbagala Mbande kata ya Mbande Temeke, majambazi ambao idadi yao haikuweza kufahamika wakiwa na silaha za moto walivamia benki ya CRDB tawi la Mbande ambapo waliwashambulia na kuwaua askari wanne wa Jeshi la Polisi waliokuwa kazini na kuwajeruhi raia wawili waliokuwa jirani na eneo hilo. 
 
Askari waliofariki katika tukio hilo ni E,5761 CPL Yahaya, F,4660 CPL Hatibu, G9524 PC Tito na G.9996 PC Gastone na raia waliojeruhiwa ni Ally Chiponda na Azizi Yahaya wote wakazi wa Mbande. 
Katika tukio hilo, majambazi hayo yalifanikiwa kupora silaha mbili za SMG na risasi sitini (60) na hakuna pesa au mali za benki iliyoibiwa, ni dhahiri kwamba walikuwa na kusudio la kujipatia silaha kwa ajili ya kufanya uhalifu na si vinginevyo kama baadhi walivyotaka kupotosha. 
Ikumbukwe kuwa majambazi mara kadhaa mwaka jana katika maeneo mbalimbali chini, mfano Kituo cha Stakishari Dar es Salaam na Kituo cha Polisi Ikwiriri , vilivyamiwa na majambazi kwa lengo la kuchukua silaha kwa ajili ya uhalifu.
 
Aidha, Tunalipongoza Jeshi la Polisi kwa kuweza kuwafikia majambazi hao huko Mkuranga bila kuumiza raia. Pia tunatoa pole kwa familia za askari wote watano waliopoteza maisha wakiwa kazini. 
Askari anaekamilsha idadi ya askari waliouwawa kufika watano ni Askari Thomas Njiku,Mkuu wa Kitengo cha Kuzuia Ujambazi alieuwa Vikindu wilayani Mkuranga wakati akiongoza kikosi maalum cha kuwasaka watu waliosadikiwa kuwa ni majambazi waliotekeleza tukio la kihalifu la Mbade,Mbagala.
 
Tunawasihi Watanzania kutoipokea dhana inayotaka kujengwa na wanasiasa kuwa hatukemei matukio haya dhidi ya polisi. 
Kumbukeni kuwa Mtandao wa Watetezi umekuwa ukitoa matamko mbali mbali kukemea mauaji ya askari wa jeshi la polisi, na tumekuwa mara kwa mara tukisisitiza kwamba askari wa jeshi la polisi ni watetezi wa haki za binadamu, kwa kuwa jukumu lao la kwanza ni kulinda mali za watu na usalama wa binadamu. 
Mtandao unatambua kuwa askari wa jeshi la polisi pia ni ndugu zetu, kaka zetu na baba zetu hivyo madhila wanayokumbana nayo ni yetu sote.
 
Mfano, katika repoti ya hali ya watetezi wa haki za binadamu kwa mwaka jana(2015) , Mtandao uliweza kuwa na kipengele maalumu kilichozungumzia haki za polisi na hali ya usalama kwa polisi wakiwa kama watetezi wa haki za binadamu.
 Katika ukarasa wa 18 wa repoti hiyo Mtandao uliweza kurekodi matukio ya uvamizi na mauaji ya jeshi la polisi zaidi ya kumi (10) na wengine watano (5) wakiachwa wamejeruhiwa. Kwa maana hii tukio lilitokea Mbagala ni muendelezo wa matukio ya kiuhalifu yanayoendelea nchini. 
 
Kumekuwa na changamoto kutoka kwa Jamii kuwatambua askari wa jeshi la polisi kama watetezi wa haki za binadamu, na hii ni kutokana na ukweli kwamba baadhi ya askari wamekuwa wakitumia vibaya madaraka yao kukandamiza haki za wananchi. 
Hali ilivyo sasa inaweza kuharibu dhana nzima ya polisi kuwa ni walinzi wa raia na mali zao, kwani vitendo wanavyofanya polisi dhidi ya raia hasa wafuasi wa vyama vya siasa na viongozi wao ni sababu kubwa ya kuharibu uhusiano mzuri kati ya polisi na raia.
 
Mtandao unatambua kwamba jeshi la polisi ni mamlaka muhimu sana katika kustawisha amani na ulinzi wa nchi kama litakuwa huru, bila kuingiliwa na wanasiasa na kuegemea upande wowote. 
Mtandao unapenda kuona kwamba Jeshi la Polisi linafanya kazi kwa weledi na kwa mujibu wa sharia na katiba ya nchi. Aidha, Mtandao unaona pamoja na migongano mbali mbali ya kazi za polisi na za wanasiasa ( hasa nafasi za wakuu wa mikoa na wilaya), ni vyema polisi wakaangalia misingi ya kimataifa ya haki za binadamu ili kuhakikisha usawa mbele ya jamii ili kurudisha mahusiano mazuri baina ya polisi na jamii wanayoitumikia.
 
Sambamba na hayo, Mtandao pia umesikikitishwa na kauli ya Mkuu wa mkoa wa Dar Es Salaam Mhe Paul Makonda aliyotoa tarehe 25 agosti 2016 wakati wa kuaga miili ya askari wanne waliouwawa huko Mbande Mkoani Dar es Salaam. Mtandao unakemea matamshi ya aina hiyo kutoka kwa kiongozi yoyote Yule, kwakuwa matamshi kama haya yanakwenda kinyume na misingi ya utawala bora na haki za binadamu na yanaweza kuwa sehemu ya kupoteza amani ya Taifa. Kitendo cha kukejeli haki za binadamu na kuamuru askari polisi wapige tu bila kujali taratibu za kisheria kinakwenda kinyume na misingi ya utawala bora.
 
Tunapenda viongozi wa serikali watambue kwamba kazi ya kulinda na kutetea haki za binadamu ni ya kikatiba na ndiyo maana kupitia Katiba yetu tuna Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iliyoundwa kwa lengo la kuhakikisha viongozi wanaheshimu misingi ya utawala bora na haki za binadamu. Watetezi wa haki za binadamu wanatambulika kote duniani na wanalindwa kisheria mfano, kimataifa tuna Tamko la watetezi wa haki za binadamu la mwaka 1998. 
 
Madhara ya Uhusiano Mbaya kati ya Polisi na Raia
Ili Jeshi la Polisi liweze kufanya kazi yake vizuri ya kupambana na uhalifu hawana budi kuhakikisha wanakuwa karibu na wananchi. Madhara ya kutokuwa na mahusiano mazuri kati ya Jeshi la Polisi na raia ni makubwa. 
 
• Mojawapo ya madhara ni pamoja na kukua kwa makosa ya jinai na polisi kukosa taarifa za waalifu toka maoneo mbalimbali.
• Hali ya makosa ya jinai Tanzania imezidi kukua katika kiwango kikubwa. Kukua kwa makosa ya jinai ni zao la kutokuwa na mahisiano mazuri kati ya raia na polisi.
Wito wetu;
• Mtandao unatoa pole kwa Jeshi la Polisi pamoja na familia za askari hao na tunatoa wito kwa askari wengine wa jeshi la polisi kuendelea na kazi zao kwa weledi huku wakiboresha mahusiano mazuri na wananchi.
• Tunaishauri serikali kuliongezea nguvu Jeshi la polisi na kuboresh utalaamu katika kufanya kazi zao
• Tunawasihi askari wa Jeshi la wananchi kuheshimu mipaka ya kazi zao na kuheshimu haki za binadamu na katiba ya nchi katika kutekeleza kazi zao za kila siku
• Tunaishauri serkali kuwe na mabadiliko katika mfumo wa jeshi la polisi kuanzia kwenye mfumo wa kisheria ambao utatoa wajibu na uwajibikaji na kuheshimu haki za binadamu
• Tunaomba umma kutoa taarifa kwa jeshi la polisi na vyombo vya usalama hasa pale wanapohisi kuna tukio linalo ashiria uvunjaji wa amani na usalama.
• Tunaiomba serikali yetu kuipa kipaumbele jeshi la polisi katika kuboresha vitendea kazi vyao,nyumba za kuishi na mishahara bora ili kukidhi hali ya maisha ya sasa.
• Tunawaomba wadau wengine wa Haki za Binadamu pamoja na mashirika mengine ya maendeleo kukemea vikali tukio hilo. Tunashauri viongozi wa siasa waache kuingilia kazi za polisi ili kuepuka migogoro
 
PICHANI  JUU :Wakili wa THRDC akiwaonyesha waandishi wa habari(hawapo pichani) repoti ambayo ilitolewa na THRDC juu ya hali ya Watetezi wa Haki za Binadamu kwa mwaka jana(2015) ,ambayo ina kipengele maalumu kilichozungumzia haki za polisi na hali ya usalama kwa polisi wakiwa kama watetezi wa haki za binadamu katika ukarasa wa 18 wa repoti hiyo, http://thrdc.or.tz/download/situation-report-2015/
 
Imetolewa na Onesmo Olengurumwa
Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC)
 
Imewasilishwa na Bennedict Ishabakaki
Wakili wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC)
 
30/08/2016

Saturday, August 27, 2016

JWTZ Lawatoa Hofu Wananchi.......Lasema Septemba 1 Litasherehekea Miaka 52 kwa Kufanya Usafi Mtaani

 
Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) leo linaanza shamrashamra za maandalizi kuelekea siku ya maadhimisho ya 52 ya majeshi inayotarajiwa kufanyika Septemba Mosi mwaka huu kwa kufanya usafi na upandaji miti katika kambi za jeshi na baadhi ya taasisi nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Dar es Salaam, Msemaji wa JWTZ Kanali Ngemela Lubinga aliwatoa hofu wananchi kuwa wasitishike pindi watakapoona wanajeshi katika maeneo ya karibu na makazi yao.

“Kesho (leo) tuaanza kufanya usafi kuanzia maeneo ya Kawe hadi karibu na kambi ya Lugalo, na kwamba niwatoe hofu wananchi pindi watakapoona wanajeshi wengi mitaani kwa kuwa hatuna nia mbaya hivyo wasitufikilie vibaya,” alisema.

Alisema jeshi hilo litafanya usafi pamoja na upandaji miti katika baadhi ya maeneo nchini hadi siku ya kilele cha maadhimisho hayo. Pia wanajeshi watajitolea damu salama katika hospitali za kambi za jeshi.

“Siku kuu ya majeshi itaadhimishwa pamoja na wanajeshi kujitolea damu kwenye vituo maalumu vya kutolea damu salama mikoani, katika hospitali zetu za kanda,” alisema na kuongeza.

“Sanjari na utoaji damu, madaktari wetu JWTZ watatoa huduma za tiba bure kama upimaji wa virusi vya Ukimwi, kisukari, na upimaji wa shinikizo la damu. “

“Kama ilivyo mila na desturi ya majeshi kufanya usafi na utunzaji wa mazingira, kuelekea siku ya maadhimisho tutafanya usafi na kupanda miti maeneo ya jirani na kambi na kwenye taasisi za kiraia kadri mahusiano yatakavyofanyika na taasisi hizo, ” alisema.

Pia alisema siku hiyo ya maadhimisho itaadhimishwa kwa kuienzi michezo na kudumisha urafiki baina ya JWTZ, wananchi, na Taasisi na kwamba mashindano mbalimbali yatafanyika.
Tarehe hiyo hiyo  ya Septemba 1 , Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetengaza kufanya maandamano na mikutano nchi nzima ili kulaani kile wanachokiita udikteta unaofanywa na serikali ya awamu ya tano.

Tayari tangazo hilo la Chadema limepingwa vikali na Rais John Magufuli, Waziri Mkuu Majaliwa Kassim, Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mambo ya Ndani na Nsato Marijani, Kamishina wa Jeshi la Polisi, Operesheni na Mafunzo huku chama hicho kikiendelea kusisitiza azma yake.