Adverts

Showing posts with label Kitaifa. Show all posts
Showing posts with label Kitaifa. Show all posts

Friday, October 7, 2016

Rais Magufuli Atangaza Kiama ....Ni cha Kuwanyang'anya Watu Wote Walioshindwa Kuendeleza Mashamba, Asisitiza Hatojali Hadhi ya Mtu

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli amewataka watu wote nchini wanaohodhi mashamba makubwa na kutoyaendeleza wafanye hivyo ndani ya mwezi mmoja kabla hayawanyang’aya mashamba hayo kwa mujibu wa sheria na mamlaka aliyonayo.

Akizungumza jana na wananchi mkoani Pwani wakati wa zoezi la kuzindua kiwanda cha kusindika matunda, Rais Dkt. Magufuli alitumia fursa hiyo kuwataka wawekezaji wanaotaka kuja nchini kuwekeza wafanye hivyo kwa kuwa ardhi ipo ya kutosha.

“Nataka watu wote wanaotaka kuja nchini kuwekeza waje, kwa kuwa ardhi ya kutosha tunayo na nawataka watu wote waliohodhi ardhi hata kama walikuwa viongozi huko nyuma nataka wayalime ndani ya mwezi mmoja na kama wasipofanya hivyo nitabatilisha hati zao za umiliki na kuwapa watu wengine ambao wapo tayari kuendeleza ardhi hiyo" Alisema Rais Dkt. John Magufuli.

Aidha Rais Magufuli alisema baadhi ya wafanyabiashara wa sukari nchini wamekuwa siyo waaminifu kwa kuagiza sukari kwa ajili ya matumizi ya viwandani kutoka nje ya nchi sukari ambayo ikifika nchini huiweka kwenye mifuko na kuiuza kwa matumizi ya kawaida ya nyumbani jambo linaloweza kuathiri afya za watumiaji.

“Tatizo la sukari liliingia baada ya kuanza kuifuatilia sukari ili sukari inayopakiwa kwa matumizi ya binadamu iwe hivyo ndipo wafanyabiashara wakaanza kuficha sukari, ndiyo maana ninataka wawekezaji waje hapa kuwekeza katika kilimo cha sukari ili sukari izalishwe hapa nchini” Alisema Rais Dkt. Magufuli.

Pamoja na hayo Rais Magufuli alikemea tabia ya watu kuficha pesa na wengine kuzigeuza katika mfumo wa dolla na kuzificha chini ya ardhi na kusisitiza wanaofanya hivyo mwisho wake watakuta pesa hizo zimeharibika huku akiwataka wazitumie kuwekeza katika viwanda.

Tuesday, October 4, 2016

Wananchi Walioua Watafiti Wakimbia Kijiji Wakihofia kukamatwa na Jeshi la Polisi........Miili Ya Marehemu Yaagwa Jijini Arusha

Baada  ya baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Iringa Mvumi katika  Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma kuwaua watafiti wa Kituo cha Udongo na Maendeleo cha Selian Arusha, wakazi wa kijiji hicho wamehama makazi yao wakihofia kukamatwa na Jeshi la Polisi.

Waandishi wa habari waliofika kijijini hapo jana na walishuhudia hali ya utulivu kijijini hapo tofauti na ilivyozoeleka.

Pamoja na wananchi hao kukimbia makazi yao, taarifa zinasema viongozi wote wa Serikali ya Kijiji hicho  wamekamatwa na polisi wakiwamo Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji, Albert Chimanga na Diwani wa Kata ya Iringa Mvumi, Robert Chikole.

Mmoja wa wakazi wa kijiji hicho aliyejitambulisha kwa jina la Michael Kagisi, alisema kitendo cha wananchi kukimbia kijiji hicho kimesababisha shughuli nyingi za  jamii kusimama   na maduka kufungwa.

Kwa mujibu wa Kagisi, hata wananchi   waliobaki kijijini hapo wakisema    hawakushiriki mauaji hayo, ikifika jioni wanakwenda porini kulala.

“Sehemu kubwa ya watu wameyakimbia makazi yao kwa sababu wanaogopa kukamatwa na polisi, yaani hata shule hazina wanafunzi kwa sababu wengi wamekimbia na wazazi wao.

“Yaani waliouawa waliuawa kwa makosa kwa sababu  kabla ya kuwapiga, walijitetea na kujitambulisha, lakini wananchi hawakutaka kuwasikiliza…   baada ya kuwaua, waliwawekea majani na kuwachoma moto ili wafe haraka,” alisema Kagisi.

Akifafanua, mwananchi huyo alisema siku ya tukio ulikuwapo mkutano kijijini hapo na mwenyekiti wa kijiji alipata taarifa kwamba katika eneo la kutengeneza chumvi, kuna gari ambalo walilitilia shaka kwamba huenda ni majambazi.

“Siku hiyo tulikuwa kwenye mkutano na baadaye tulimuona mwenyekiti akiwaita baadhi ya vijana na kuwaagiza waende eneo la tukio.

“Wale vijana walikwenda huko  walipiga simu kijijini kuwaeleza wananchi, kwamba kuna gari la watu ambao hawaeleweki.

“Taarifa hizo ziliposambaa, wananchi walihamasishana na kuelekea eneo la tukio.

“Walipofika tu, walianza kuwapiga, lakini wale watafiti walijieleza kwamba wao siyo majambazi, huku wakiwaomba wananchi wawapeleke katika ofisi zao za kijiji, lakini wananchi walikataa na kuendelea kuwapiga hadi walipowaua,” alisema.

Naye  Mchungaji wa Kanisa la Biblia kijijini hapo, Donald Nyambuya, alisema kwa sasa maisha kijijini hapo ni ya shida kwa sababu huduma nyingi za  jamii zimefungwa baada ya watu kukimbia makazi yao.

Mwinjilisti wa Kanisa la Waadventista Wasabato (SDA), Jacob Foda, alisema kitendo cha watu kukimbia makazi yao  kimeathiri huduma ya  roho kwa kuwa huwa na kawaida kuwatembelea waumini wake.

Wakati huohuo, simanzi na majonzi, jana, vilitawala wakati wa kuaga miili ya Watafiti wa Kituo cha Utafiti wa Udongo na Maendeleo cha Selian mjini hapa.

Watafiti hao waliuawa juzi na wananchi wa Kijiji cha Iringa Mvumi, wilayani Chamwino, Mkoa wa Dodoma kwa kukatwakatwa mapanga na kuchomwa moto.

Miili hiyo iliwasili mjini hapa jana asubuhi kwa gari ikitokea Dodoma na kuingizwa kwenye eneo la wazi la kituo hicho kilichopo pembeni mwa Uwanja mdogo wa Ndege wa Arusha kwa ajili ya wafanyakazi kutoa heshima za mwisho.

Shughuli ya kuaga miili hiyo ilifanyika asubuhi kwa wafanyakazi, jamaa na marafiki kutoa heshima za mwisho bila majeneza kufunguliwa kwa kuwa imeharibika.

Baadaye  ilipelekwa katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru kwa ajili ya kufanyiwa maandalizi ya kusafirishwa.

Waliouawa katika tukio hilo  walitambuliwa kuwa ni Jaffari Mafuru aliyesafirishwa jana kwenda Mara kwa mazishi, Theresia Ngume, aliyetarajiwa kuzikwa jana mjini Arusha na dereva wa gari walilokuwamo,       STJ 9570 aina ya Toyota Hilux, mali ya Kituo cha Utafiti cha Selian, Nikas Magazine, aliyesafirishwa kwenda Ifakara, Morogoro kwa mazishi.

Watafiti hao  waliuawa wakiwa katika kazi ya mradi unaoandaa taarifa za hali ya udogo kwa nchi nzima.

Akizungumza baada ya kutoa heshima za mwisho, Mkurugenzi wa Kituo hicho, Januari Mafuru ambaye ni baba mzazi wa marehemu Jaffari, alisema tukio hilo limemuumiza sana.

Alisema kituo hicho kimekuwa kikiendesha mradi huo kwa lengo la kuwasilisha taarifa hizo kwa wakulima wadogo na wataalamu wa kilimo  ziweze kuwasaidia wananchi katika kilimo na hatimaye kuongeza mazao.

“Mradi huu umemaliza utafiti katika Mikoa ya Kanda ya Kaskazini ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara. Baada ya hapo kazi nyingine ilikuwa imeanza Kanda ya Kati Dodoma na Singida.

“Wiki iliyopita, tuliandaa watafiti wanane na magari yao manne kwa ajili ya kwenda mkoani Dodoma kukusanya udongo kwa ajili ya kuuleta hapa kwenye maabara za Seliani kufanyiwa utafiti kisha kutoa matokeo yatakayowarudia wakulima,” alisema Mafuru.

Akizungumzia kuwasili kwa watafiti hao katika Kijiji cha Iringa Mvumi, wilayani Chamwino yalikotokea mauaji hayo, Mafuru alisema timu zote zilikuwa na barua za utambulisho pamoja na vifaa vya kazi.

“Timu iliyokuwa Chamwino katika Kijiji cha Iringa Mvumi, iliwakuta wanawake wakiendelea na shughuli za kukusanya chumvi  na watafiti waliwasilimia na kujitambulisha wametokea wapi.

“Taarifa tulizonazo ni kwamba, baada ya kusalimia, watafiti waliacha gari pembeni na kutembelea maeneo   kuchagua udogo.

“Huku nyuma kundi la wale wanawake lilitoa taarifa kwa viongozi wao kuwa wamevamiwa na wanyonya damu, ndipo walipotokea watu wakiwa na mashoka na mapanga na   kuwashambulia kabla ya kuwachoma moto,” alisema.

Mtafiti Mwandamizi wa Kituo cha Selian, Dk. Lameck Makoye, alilaani mauaji hayo na kusema hajawahi kuona wala kusikia watafiti wakivamiwa   wanapokuwa   vijijini.

“Naamini Serikali imeona, binafsi sijawahi kuona tukio la aina hii kwa sababu  watafiti wale walikuwa na vielelezo vyote vinavyowatambulisha.

“Hata mradi waliokwenda kufanya ulikuwa ni kwa faida ya wananchi wa Kijiji cha Iringa Mvumi kwa vile umelenga maeneo ya nchi nzima.

“Sisi Kituo cha Utafiti cha Selian ndiyo tunaoleta maendeleo ya mkulima kwa nchi nzima kwa kufanya utafiti wa udongo unaomwezesha mkulima alime vipi na atumie mbolea kwa kiwango gani na ya aina gani,” alisema Dk. Makoye.

Mume wa marehemu Theresia, Jonas Mjema, akizungumza kwa huzuni kuhusu  kuondokewa na mkewe, alisema kabla ya tukio la mkewe kuchomwa moto, alizungumza naye asubuhi kujua anaendeleaje.

“Niliwasiliana naye asubuhi Jumamosi tukatakiana kazi njema, ilipofika jioni nilimtafuta lakini simu yake haikupatikana.

“Nilijipa matumaini labda mawasiliano hayakuwa mazuri kwa vile shughuli zao ni za porini.

“Ilipofika Jumapili, nilipigiwa simu na shemeji yangu akinipa taarifa za tukio la kuchomwa moto mke wangu,” alisema Mjema aliyeachwa na watoto wawili.

Monday, October 3, 2016

Rais Magufuli Akutana Na Makamu Wa Rais Wa Jamhuri Ya Cuba, Ikulu Jijini Dar Leo

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 03 Oktoba, 2016 amekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa Cuba Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa ambapo viongozi hao wamekubaliana kuimarisha na kuongeza uhusiano na ushirikiano kati ya nchi hizi mbili kwa manufaa ya wananchi wake.

Katika Mazungumzo hayo Rais Magufuli amesema anatambua uhusiano na ushirikiano mzuri na wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Cuba na kwamba Serikali yake imejipanga kuhakikisha uhusiano huu unaelekezwa katika maeneo yenye manufaa ya kiuchumi na ustawi wa jamii.

Rais Magufuli amemuomba Makamu huyo wa Rais wa Cuba kuwashawishi wawekezaji wa kutoka nchini mwake kuja hapa nchini kujenga viwanda vya kutengeneza dawa za binadamu ili kurahisisha upatikanaji wa dawa na kupunguza gharama.

Pia, Rais Magufuli amemuomba Makamu wa Rais wa Cuba Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa kuwashawishi wafanyabiashara wa Cuba kuja kuwekeza katika uzalishaji wa sukari na amewahakikishia kuwa wakiwa tayari Serikali ya Tanzania ipo tayari kuwapa ardhi kwa ajili ya kuendesha uzalishaji huo.

"Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa najua kuwa nchi yenu ina utaalamu wa kutosha katika uzalishaji wa sukari, uzalishaji wa dawa za binadamu na masuala mengine mengi yanayohusu matumizi ya teknolojia katika shughuli mbalimbali za uzalishaji, nakuomba uwaambie wafanyabiashara wa Cuba kuwa tunawakaribisha waje Tanzania kuwekeza na Serikali itawapa ushirikiano wa kutosha" amesema Rais Magufuli.

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa Cuba Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa amempongeza Rais Magufuli kwa juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali yake katika kuinua uchumi wa Tanzania na amemhakikishia kuwa Cuba ipo tayari kushirikiana na Tanzania kwa kutumia utaalamu na uzoefu wake.

Amesema kwa kuanzia Cuba italeta wataalamu kwa ajili ya kuangalia namna itakavyotekeleza ombi la kujenga viwanda vya kutengeneza dawa za binadamu na pia atazungumza na Jumuiya ya Wafanyabiashara wa Cuba na kuwashawishi kuja hapa nchini kuwekeza katika uzalishaji wa sukari.

"Mhe. Rais Magufuli natambua kuwa uhusiano wetu na Tanzania na Afrika ni wa kihistoria, sisi Cuba tumepiga hatua kubwa katika maendeleo ya uchumi na teknolojia, nimekuja kukuhakikishia kuwa tutauendeleza uhusiano huu ili ulete manufaa kwenu na kwa wananchi wa Cuba" amesema Mhe. Mesa.
 

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
03 Oktoba, 2016

Thursday, September 1, 2016

Rais Dkt. Magufuli Awapongeza JWTZ Kwa Kutimiza Miaka 52 Tangu Kuanzishwa Kwake

Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuwaunga mkono na kuwatumia wahandisi wa ndani wenye ujuzi mbalimbali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa viwanda, reli, barabara na miundombinu mingine.

Hayo yamesema na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, alipokuwa akifungua Mkutano wa 14 wa mwaka wa wahandisi unaofanyika kwa siku mbili kuanzia leo tarehe 01 Septemba, 2016 katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.
 
Dkt. Magufuli amesema atafurahi kuona miradi inayohusisha kazi za kihandisi na hasa wakati huu ambapo nchi inaelekea katika uchumi wa viwanda inatekelezwa kwa kutumia wahandisi wa ndani na hivyo amewataka kujipanga sawasawa ili kukabiliana na changamoto hiyo.

"Nyinyi wahandisi mkiamua nchi hii iende kwenye uchumi wa kati tutafika, mkiamua nchi hii iende kwenye uchumi wa viwanda tutafika, na msipoamua hatutafika. 
 
"Sasa hivi kuna ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (Standard gauge) kwani nyinyi mnashindwa kujenga?" Amehoji Rais Magufuli huku akisisitiza kuwa Serikali yake ipo tayari kuwaunga mkono pale watakapohitaji msaada.
 
Hata hivyo Dkt. Magufuli amewakumbusha umuhimu wa kufanya kazi kwa ubora, ushirikiano na upendo miongoni mwao huku akielezea kusikitishwa kwake na baadhi ya wahandisi ambao wamekuwa wakifanya vitendo vya ukiukwaji wa maadili ikiwemo kushirikiana na wakandarasi na wazabuni kuzidisha viwango vya makadirio ya gharama za miradi na manunuzi ya Serikali ili kujipatia fedha isivyo halali na kupitisha miradi iliyojenga chini ya viwango.
 
Rais Magufuli ameongeza kuwa Serikali yake itaendelea kuchukua hatua kali dhidi ya wote wanaotumia vibaya fedha za umma na amesisitiza kuwa hatua zaidi za kuhakikisha kunakuwa na nidhamu katika matumizi ya fedha za Serikali zitachukuliwa.
 
"Kuna watu wanasema mzunguko wa pesa umepungua na hali imekuwa ngumu, hizo pesa zilizokuwa zinachezewa huko mitaani zilikuwa pesa za Serikali, mimi nataka pesa ziende kwenye miradi ya maendeleo na ndio maana bajeti ya maendeleo tumeongeza kutoka asilimia 26 hadi asilimia 40" Amesisitiza Rais Magufuli.
 
Katika tukio jingine, Rais Magufuli amewatembelea Askari wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) Kikosi cha 603 (Air Wing) kilichopo Ukonga Jijini Dar es Salaam na kuwapongeza kwa kuadhimisha miaka 52 ya tangu kuanzishwa kwa Jeshi hilo. 
 
Katika kuadhimisha miaka 52 ya JWTZ Askari wa Jeshi hilo wamefanya usafi katika maeneo mbalimbali.
 
Pamoja na pongezi hizo Rais Magufuli amekagua baadhi ya ndege zinazotumiwa na Jeshi hilo na amewahakikishia Wanajeshi kuwa Serikali yake itaendelea kuliimarisha Jeshi hilo kwa vifaa na maslai ya Askari ili kuendelea kuwa na Jeshi bora, la kisasa na lililo tayari kuilinda nchi wakati wote. 
 
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es Salaam
01 Septemba, 2016

Wednesday, August 31, 2016

Rais Magufuli apongezwa kwa kupambana na rushwa na kujenga mazingira bora zaidi kwa uwekezaji nchini

 
Mwenyekiti wa Taasisi inayoshughulikia masuala ya Afrika (Africa Matters Limited) Mhe. (Baroness) Lynda Chalker wa Wallasey - Uingereza, amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa juhudi kubwa alizozifanya kupiga vita rushwa na kujenga mazingira bora zaidi kwa uwekezaji.

Mhe. Lynda Chalker ametoa pongezi hizo jana tarehe 31 Agosti, 2016 Ikulu Jijini Dar es Salaam alipokutana na kufanya mazungumzo na Rais Magufuli kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo hali ya uwekezaji hapa nchini.

"Mhe Rais amefanya uamuzi sahihi wa kupiga vita rushwa na kuiweka nchi hii katika njia mpya ya uwekezaji mzuri na hicho ndicho tumekuwa tukikizungumza, nimejitahidi kutoa ushauri wangu wa namna mimi na kampuni yangu binafsi tunaweza kumsaidia, nionavyo mambo yanakwenda katika mwelekeo mzuri" Amesema Mhe. Lynda Chalker.

Kwa Upande wake Rais Magufuli amemshukuru Mhe. Lynda Chalker kwa ushauri na dhamira yake ya kutaka Tanzania ipige hatua kimaendeleo na amemuomba kutumia ushawishi wake kuwahamasisha wawekezaji mbalimbali kutoka nchini Uingereza na kwingineko duniani kuja kuwekeza nchini Tanzania ili kuharakisha zaidi maendeleo.

Hata hivyo Dkt. Magufuli amesema wawekezaji wanaokuja Tanzania hawana budi kuwa wawekezaji makini.

"Ninawakaribisha wawekezaji makini kutoka Uingereza na mahali popote dunia, lakini nisingependa kupata wawekezaji wababaishaji" Amesisitiza Rais Magufuli.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es Salaam
31 Agosti, 2016

Tuesday, August 30, 2016

Rais Magufuli kufungua maadhimisho ya wahandisi

Msajili wa Bodi ya Wahandisi nchini (ERB), Eng. Steven Mlote akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani), kuhusu maadhimisho ya 14 ya Siku ya Wahandisi Tanzania itakayoadhimishwa Septemba mosi jijini Dar es Salaam.(Picha Zote Na Benjamin Sawe – Maelezo).
****

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya kumi na nne ya Siku ya Wahandisi yatakayofanyika Septemba mosi hadi pili jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo ya siku mbili yanatarajiwa kukutanisha zaidi ya wahandisi elfu mbili kutoka ndani na nje ya nchi ili kupata fursa ya kufanya majadiliano ya kitaaluma, kufanya maonesho ya kiufundi na kibiashara, kuwatambua na kuwazawadia wahandisi wahitimu waliofanya vizuri katika mafunzo yao ya mwisho na kuwaapisha wahandisi waliokidhi vigezo.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Msajili wa Bodi ya Wahandisi nchini (ERB), Eng. Steven Mlote amesema mada kuu katika maadhimisho hayo itakuwa ni “TANZANIA KUELEKEA KUWA NCHI YA UCHUMI WA KATI NA KUWA NCHI YA VIWANDA: NINI JUKUMU LA WAHANDISI”.

“Tumejipanga Siku ya Wahandisi mwaka huu iwe na mvuto wa pekee kwa sababu mada yake ni ya kitaifa ikiangalia Dira ya Maendeleo ya Taifa na mwelekeo wa nchi kuwa nchi ya viwanda” amesema Eng. Mlote.

Maadhimisho ya wahandisi Tanzania yamekuwa yakifanyika tangu mwaka 2013, lengo likiwa ni kuiwezesha jumuiya ya wahandisi nchini kuionesha jamii kile ambacho wahandisi wanaweza kukifanya katika kuleta maendeleo ya nchi.

Takribani wahandisi elfu 17 wanakadiriwa kuwepo nchini katika sekta mbalimbali, lengo likiwa ni kuwa na wahandisi elfu 83 ili kukidhi mahitaji ya nchi kuwa ya kipato cha kati ifikapo mwaka 2025.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Saturday, August 27, 2016

JWTZ Lawatoa Hofu Wananchi.......Lasema Septemba 1 Litasherehekea Miaka 52 kwa Kufanya Usafi Mtaani

 
Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) leo linaanza shamrashamra za maandalizi kuelekea siku ya maadhimisho ya 52 ya majeshi inayotarajiwa kufanyika Septemba Mosi mwaka huu kwa kufanya usafi na upandaji miti katika kambi za jeshi na baadhi ya taasisi nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Dar es Salaam, Msemaji wa JWTZ Kanali Ngemela Lubinga aliwatoa hofu wananchi kuwa wasitishike pindi watakapoona wanajeshi katika maeneo ya karibu na makazi yao.

“Kesho (leo) tuaanza kufanya usafi kuanzia maeneo ya Kawe hadi karibu na kambi ya Lugalo, na kwamba niwatoe hofu wananchi pindi watakapoona wanajeshi wengi mitaani kwa kuwa hatuna nia mbaya hivyo wasitufikilie vibaya,” alisema.

Alisema jeshi hilo litafanya usafi pamoja na upandaji miti katika baadhi ya maeneo nchini hadi siku ya kilele cha maadhimisho hayo. Pia wanajeshi watajitolea damu salama katika hospitali za kambi za jeshi.

“Siku kuu ya majeshi itaadhimishwa pamoja na wanajeshi kujitolea damu kwenye vituo maalumu vya kutolea damu salama mikoani, katika hospitali zetu za kanda,” alisema na kuongeza.

“Sanjari na utoaji damu, madaktari wetu JWTZ watatoa huduma za tiba bure kama upimaji wa virusi vya Ukimwi, kisukari, na upimaji wa shinikizo la damu. “

“Kama ilivyo mila na desturi ya majeshi kufanya usafi na utunzaji wa mazingira, kuelekea siku ya maadhimisho tutafanya usafi na kupanda miti maeneo ya jirani na kambi na kwenye taasisi za kiraia kadri mahusiano yatakavyofanyika na taasisi hizo, ” alisema.

Pia alisema siku hiyo ya maadhimisho itaadhimishwa kwa kuienzi michezo na kudumisha urafiki baina ya JWTZ, wananchi, na Taasisi na kwamba mashindano mbalimbali yatafanyika.
Tarehe hiyo hiyo  ya Septemba 1 , Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimetengaza kufanya maandamano na mikutano nchi nzima ili kulaani kile wanachokiita udikteta unaofanywa na serikali ya awamu ya tano.

Tayari tangazo hilo la Chadema limepingwa vikali na Rais John Magufuli, Waziri Mkuu Majaliwa Kassim, Mwigulu Nchemba, Waziri wa Mambo ya Ndani na Nsato Marijani, Kamishina wa Jeshi la Polisi, Operesheni na Mafunzo huku chama hicho kikiendelea kusisitiza azma yake.

Friday, August 26, 2016

Waziri Simbachawene Aagiza Machinga waondolewe Kariakoo....Asema Rais hakumaanisha warudi


Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuwaondoa wafanyabiashara wadogo maarufu kama Machinga katika maeneo ya soko la Kariakoo na barabarani, hususan karibu na barabara za mabasi ya mwendo kasi.

Akizungumza jana na Kamati ya Bunge, Waziri huyo wa TAMISEMI alisema kuwa kurejea kwa wafanyabiashara hao katika maeneo hayo kumeleta usumbufu mkubwa na uchafu wa mazingira katika maeneo ya jiji.

“Namuagiza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam awaondoe na asilegeze kamba,” alisema Waziri Simbachawene.

Alisema kuwa hali hiyo imetokana na tafsiri isiyo sahihi ya agizo la Rais John Magufuli alipokuwa ziarani Mkoani Mwanza.

“Wala agizo  la Mheshimiwa Rais halikumaanisha hicho. Mheshimiwa Rais alisema tuwatafutie maeneo mbadala ambao wapo maeneo kama ya Mwanza na walikuwa wanafanya biashara ya kuuza nguo, akizungumzia wale particular group walioko pale Mwanza. Kwa Dar es Salaam tulishamaliza huko,” alisema.

Aidha, alimtaka Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kuhakikisha hakuna hata machinga mmoja atakayeonekana akifanya biashara katika maeneo ya barabara za mabasi yaendayo kasi.

Aigizo hilo la Waziri Simbachawene liliungwa Mkono na wajumbe wa Kamati hiyo ya Bunge ambao walisema kuwa hali ya soko la Kariakoo imekuwa mbaya kutokana na kuzagaa kwa machinga.

Polisi Mwingine Auawa Kwenye Mapambano Makali na Majambazi Huko Mkuranga

 
Ilikuwa ni kama filamu ya askari na maadui wakati askari wa Jeshi la Polisi walipopambana na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi kwenye nyumba iliyo eneo la Vikindu wilayani Mkuranga.

Taarifa ambazo zimepatikana kutoka kwa watu waliokuwa karibu na operesheni hiyo na ambazo hazijathibitishwa na mamlaka rasmi, zinasema kamishna wa Kitengo cha Kuzuia Ujambazi, ASP Thomas Njuki aliuawa kwa kupigwa risasi kichwani. 
Taarifa hizo zilisema kuwa jambazi mmoja aliuawa ingawa idadi ya waliokamatwa haikufahamika mara moja kutokana na mashuhuda kutoa takwimu tofauti. 
Kamanda wa Polisi wa Kanda maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro alisema ataongea na waandishi wa habari leo saa 4:00 asubuhi kuzungumzia tukio hilo. 
Tukio hilo limetokea siku chache baada ya askari wanne wa Jeshi la Polisi kuuawa wakati wakibadilishana lindo kwenye tawi la benki ya CRDB lililoko Mbande jijini Dar es Salaam. 
Watu hao, waliofika wakiwa wamepanda pikipiki, walipora silaha na kutoweka nazo. Katika tukio la jana, askari wa Jeshi la Polisi walikuwa na nia ya kuwakamata watu waliowashuku kuwa ni majambazi. 
Kwa mujibu wa watu wanaoishi karibu na nyumba hiyo, mpambano kati ya polisi na majambazi hao ulianza saa 7:30 usiku baada ya polisi kuvamia nyumba walimopanga majambazi hayo. 
Tukio lilivyotokea 
Chanzo kimoja cha habari kimeeleza kuwa baada ya polisi kufuatilia nyendo za wakazi wa nyumba hiyo walianza upelelezi na kubaini kuwa huenda wanahusika na matukio kadhaa ya uhalifu, likiwamo la uvamizi wa kituo cha polisi cha Stakishari na lile la tawi la CRDB Mbande mkoani Pwani. 
Mpashaji huyo alisema kuwa jana saa saba usiku, polisi walifika kwenye nyumba hiyo iliyo Mtaa wa Vikindu Mashariki ambayo ina maduka upande wa mbele, ikipakana na nyumbani nyingine mbili pembeni na nyuma zikiwa umbali usiozidi hatua nne. 
Habari hizo zinasema askari hao kwanza walimtuma mwenyekiti wa serikali ya mtaa kwenda kuwasihi wafungue mlango na walipokataa ndipo walipoenda kugonga, wakiwaamrisha watu hao wafungue mlango. 
“Baada ya kuona hawatii amri ya kufungua mlango, polisi waliamua kuvunja vitasa kwa kutumia bastola, ndipo risasi zikaanza kurushwa,” alisema mpashaji habari huyo. 
 “Kwa kuwa mkuu alikuwa mbele, wahalifu walimpiga risasi kichwani na alikufa palepale.” 
Mtu huyo alisema kuwa baada ya Kamishna Njuki kufariki, askari wengine walirudi nyuma kujihami zaidi. 

Baada ya hapo polisi waliendelea kupiga risasi kuelekea maeneo mbalimbali ya nyumba hiyo na wahalifu hao kujibu mashambulizi. 

“Kila chumba ambacho polisi walikuwa wakijaribu kurusha risasi, zilijibiwa. Inaelekea kila chumba kilikuwa na mtu mwenye silaha,” alisema shuhuda mwingine wa tukio hilo. 

Habari kutoka kwa majirani zinasema hadi saa 2:45 asubuhi, milio ya risasi iliendelea kurindima katika eneo hilo. 
Baadaye polisi waliomba kuongezewa nguvu na Jeshi la Wananchi (JWTZ) ambao walifika na kuendeleza mapambano hayo. 

 Mtoto ataja alipojificha baba
Wakati mapambano yakiendelea, sauti za watoto waliokuwa wakilia zilisikika na ndipo askari wa JWTZ waliamuru watu hao wawatoe nje. 
“Watoto walipotoka nje, polisi waliwauliza baba yupo wapi, mtoto mmoja akajibu yupo darini,” alisema

Baada ya polisi kusikia hivyo, walielekeza mashambulizi yao darini na kufanikiwa kumjeruhi mtu aliyejificha darini ambaye alishuka. 

Wakati polisi wakishinikiza atoke ndani ili kujisalimisha, mtu huyo alijipiga risasi mara baada ya kutoka na kufariki dunia.
Wakazi Vikindu wahaha!
Kutokana na tukio hilo, taharuki ilitanda kwa wakazi wa Vikindu na biashara zote zilifungwa eneo hilo huku wananchi wakiwa na chupa za maji kutokana na mabomu ya machozi yaliyokuwa yakipigwa kila mara. 
Wakazi wa eneo ambalo lipo karibu na maegesho ya magari ya Farid Seif, hawakuruhusiwa kutoka ndani na waliofanikiwa kutoka usiku hawakuingia hadi jana saa 7.00 mchana wakati hali ilipotulia. 
Kutokana na majibizano ya risasi, watu wanaofanya kazi jijini Dar es Salaam ambao wanaishi vijiji vya Melela, Vianzi, Pemba Mnazi na Mfuru hawakwenda kazini kutokana na barabara inayotoka Vikindu kufungwa hadi saa 7.00 mchana. 
Tukio hilo lilisababisha umati wa watu kukusanyika kushuhudia mapambano hayo, lakini hakuna raia aliyeruhusiwa kuvuka mita 150 kwenda eneo la tukio. 
Nyumba waliokuwa Wanaishi hao Majambazi

Sunday, April 3, 2016

Halima Mdee Amtaka Rais Magufuli Ataje Posho na Marupurupu Anayolipwa


Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), Halima Mdee amemuomba Rais John Magufuli kuweka wazi posho na marupurupu anayoyapata ili Watanzania wajue kiasi halisi anachokipata mbali na mshahara wake.

Mdee ambaye ni mbunge wa Kawe, alitoa ombi hilo jana kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Sokoni, Jimbo la Mtama mkoani Lindi, uliohudhuriwa na mamia ya wananchi wa jimbo hilo.

Kauli hiyo ya Mdee imekuja siku moja baada ya Rais Magufuli kutaja mshahara wake kuwa ni Sh9.5 milioni kwa mwezi. 
“Juzi Rais anasema eti mshahara wake Sh9.5 milioni, sasa atutajie posho za kila siku ili kila Mtanzania ajue kiasi ambacho anakipata,” alisema Mdee.

Mdee aliongeza kuwa wabunge wanalipwa mshahara wa Sh3 milioni, lakini kuna posho mbalimbali kutokana na kuhudumia wananchi.

“Sisi wabunge mshahara wetu katika hati ya mshahara unasomeka Sh3 milioni, lakini posho na pesa ya mambo ya utendaji ya mbunge inafika Sh10 milioni, Rais atuambie na yeye posho zake ni kiasi gani,” alisema Mdee.

Mbunge wa Jimbo la Ndanda katika Wilaya ya Masasi, Cecil Mwambe alidai katika mkutano huo kuwa wananchi wa Mtama wamekosa mwakilishi wa kuwasemea matatizo yao, hasa ya upande wa kilimo cha korosho kutokana na mbunge wao, Nape Nnauye kukosa uwezo wa kusimama bungeni kuisema Serikali.

“Mtama mmekosa mwakilishi, hapa kuna tatizo la korosho na mbunge aliyepo anashindwa kulisemea, hivyo mtabaki hivyo hivyo bila kutatua tatizo lenu kwa kipindi cha miaka mitano,” alidai Mwambe.

Mzimu Wazidi Kumuandama Mbunge Wa CCM Suleiman Saddiq Murad.....Baada ya TAKUKURU Kumpandisha Kizimbani, TBS Nao Wavamia Bekari Yake


Mzimu umeendelea kumwandama Mbunge wa Mvomero, Suleiman Saddiq Murad. 
Baada  ya  TAKUKURU  kumpandisha  mahakamani wiki iliyopita  kwa kuomba rushwa ya milioni 30, shirika la Viwango Tanzania (TBS)  nalo limeifunga Bekari yake( tanuri mikate )   kwa muda usiojulikana kwa kutotimiza masharti  ya viwango vya ubora.

Tanuri mikate hiyo pamoja na zingine 3 za watu wengine zilizopo Mkoani Morogoro, zilikaguliwa kwa mara ya kwanza Julai mwaka jana na wamiliki wake kupewa muda wa miezi sita kurekebisha kasoro zilizokuwepo, lakini hadi Machi 10, mwaka huu katika ukaguzi mwingine walikuwa hawajatekeleza na kutimiza masharti yaliyotolewa na TBS.

Mkaguzi wa TBS, Ashura Katunzi alisema kazi ya kuzifungia tanuri mikate hizo ipo kisheria baada ya wamiliki wake kushindwa kufuata utaratibu walioelekezwa awali wa kurekebisha kasoro kabla ya kuanza kwa uzalishaji tena.

Katunzi ambaye pia ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Udhibiti wa Ubora wa TBS, alisema: “Kabla ya kufunga bekari hizi, wakaguzi wa TBS walizitembelea tena mnamo Machi 10, mwaka huu ili kujiridhisha na iwapo utekelezaji umefanyika katika kipindi cha miezi sita waliopewa, lakini hakuna kilichofanyika,” alisema Katunzi juzi wakati wakifanya ukaguzi na kuchukua uamuzi huo.

Alisema kutokana na kukaidi agizo hilo, TBS imezifungua kwa muda usiojulikana hadi watakaporekebisha kulingana na maelekezo na kuomba upya kufunguliwa baada ya ukaguzi mwingine kufanyika.

Tanuri mikate zilizofungiwa kuanzia juzi ni MS Bakery Magooma Super Market inayomilikiwa na Murad, Baraka Bakery mali ya Salim Nassor, Sifasita Bakery inayomilikiwa na Tanzua Tambi na M&M Bakery mali ya Sarah Sanya.

“Bekari hizi zimekutwa zinafanya kazi katika mazingira hatarishi yasiyo salama na yanatia hofu kwa mlaji, zina ukosefu wa vyoo, zipo kwenye makazi ya watu na ukosefu wa vyumba vya kubadilisha nguo kwa wafanyakazi,” alifafanua Katunzi na kuongeza:
 “Katika ukaguzi wetu tumeona bekari hizi zina ukosefu wa eneo maalumu la kuoshea vyombo, uchakavu wa sakafu, mikate kuwekwa sakafuni na ufinyu wa eneo la kazi.”

Alisema endapo wamiliki hao watarekebisha kasoro na kutimiza viwango vya ubora, wanatakiwa kuwasilisha tena maombi rasmi TBS ili wakaguliwe tena ili kujiridhisha iwapo wametimiza vigezo kabla ya kufunguliwa tena.

“Watakapoharakisha kufanya marekebisho waliyoelelezwa, ndipo watakapoweza kufunguliwa haraka kuendelea na uzalishaji tena,” alifafanua mkaguzi huyo wa shirika la viwango.

Naye Ofisa Uhusiano wa TBS, Roida Andusamile alisema licha ya kuzifungia tanuri mikate hizo, kazi hiyo inaendelea ili kuzifikia nyingine zilizokaguliwa na kushindwa kutekeleza masharti yake.

Hivyo alitoa mwito kwa wazalishaji wa mikate katika Manispaa ya Morogoro na maeneo mengine wafuate utaratibu na kuweka ubora wa mikate kwa kuzingatia viwango vya TBS kabla ya kufikisha sokoni kwa walaji.

Baadhi ya wafanyakazi waliokutwa katika tanuri mikate hizo waliwasihi wakaguzi wa TBS wasiwafungie na badala yake wawapatie muda wa ziada ili warekebishe kasoro hizo wakati wakiendelea na uzalishaji, maombi yaliyogonga mwamba kutokana na kufungwa kwa milango kwa makomeo chini ya ulinzi wa Polisi.

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga amkamua jipu Mhandisi wa manispaa....Amsweka Rumande huku Mkurugenzi wake Akishuhudia

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro amemsweka rumande Muhandisi wa halmashauri ya manispaa ya Shinyanga Simoni Ngagani, baada ya kupuuza agizo lake la kufanya maandalizi mapema ya kununua kokoto na Saruji kwa ajili ya kusimika mapipa 50 ya kutunzia uchafu kwenye mitaa mbalimbali katika manispaa ya Shinyanga ikiwemo eneo la kituo cha mabasi yaendayo wilayani.

Tukio hilo limetokea juzi asubuhi mjini Shinyanga wakati mkuu huyo wa wilaya akiwa na msafara wake alipowasili katika eneo la stendi ya mabasi yaendayo wilayani kwa lengo la kufanya uzinduzi wa kusimikwa kwa mapipa hayo na kukuta maandalizi hayajakamilika.

Matiro alimuagiza Mhandisi huyo kufanya maandalizi hayo mapema mbele ya mkurugenzi wake wa manispaa ya Shinyanga Kalinjuna Lewis, kuwa ataandaa vifaa hivyo majira ya saa moja asubuhi ili zoezi la  kusimika mapipa hayo likamilike haraka, na baada ya hapo wafanye usafi wa mazingira lakini agizo hilo lilipuuzwa na mhandisi huyo .

Mkuu huyo alipomhoji mhandisi kwanini alipuuzia agizo lake la kufanya maandalizi mapema, mhandisi huyo alisema sababu iliyomkwamisha ni kukosekana kwa pesa za kununua kokoto na saruji kwani mvua kubwa ilinyesha na kushindwa kwenda benki, na alivyoamka asubuhi ndipo atakafuta dhana hizo.

Hata hivyo mkuu huyo hakuridhika na majibu hayo ndipo DC alipochukua uamuzi ya kumsweka rumande kwa kumuagiza mkuu wa kituo cha polisi wilaya ya Shinyanga kumkamata na kumuweka ndani mhandisi huyo wa ujenzi manispaa hiyo Samson Ngagani kwa kosa la kuchelewesha maandalizi ya vifaa vya ujenzi vilivyopangwa kutumika kusimika mapipa ya taka.

“Haiwezekani tukubaliane tuamke mapema ili tufanye kazi hii haraka na pia tuingie Mitaani kufanya usafi, ambapo mimi nimeamka saa 11 nikajiandaa harafu wewe una kuja saa mbili tena bila ya kufanya maandalizi yeyote hii ni kunidharau, hivyo naagiza OCD mkamate akakae Rumande kwanza ili liwe fundisho kwa wengine” ,alisema Matiro.

Katika uzinduzi huo Matiro alisema mapipa hayo ya taka ambayo idadi yake ni zaidi ya 50 yatawekwa katika maeneo mbali mbali ya manispaa ya Shinyanga na wananchi wanatakiwa kuyalinda. 
Awali akiongea katika uzinduzi huo, mkurugenzi wa manispaa ya Shinyanga Lewis Kalinjuna alisema mapipa hayo yamepatikana kutokana na wadau mbali mbali kujitolea kuchangia baada ya kuhamasishwa na mkuu huyo wa wilaya ambapo pipa moja limegharimu shilingi elfu 90.

Naye afisa afya wa manispaa ya shinyanga Elly Nakuzelwa alisema lengo la kuweka mapipa hayo ya taka ni kuhakikisha manispaa ya Shinyanga inakuwa katika hali ya usafi ili kuondoa magonjwa ya miripuko yanayosababishwa na uchafu ikiwemo kipindupindu. 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akimhoji Mhandisi wa ujenzi wa manispaa ya Shinyanga Simon Ngagani (katikati mwenye kaunda suti)kwa kupuunza agizo lake la kufanya maandalizi mapema ya kununua vifaa vya ujenzi vya kusimikia Mapipa ya uchafu 50 katika mitaa mbalimbali ya Mji wa Shinyanga ,na mwenye traksuti kushoto ni Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Kalinjuna Lewis akishuhudia Mtumishi wake akikamuliwa Jipu na hatimaye kuswekwa rumande kwa kumpuuza DC huyo