Adverts

Friday, October 7, 2016

Mamlaka ya Mapato (TRA): Makusanyo ya Kodi mwezi Septemba 2016

 
Mkurugenzi wa Elimu na huduma kwa mlipa kodi wa TRA, Bw. Richard Kayombo amesema mwenendo wa ukusanyaji mapato ya Serikali kwa sasa ni wa kuridhisha katika  kufikia  lengo la kukusanya kiasi cha shilingi trioni 15.1 kwa mwaka fedha wa 2016/2017.

Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) imekusanya Mapato ya shilingi trilioni 1.37 kwa Mwezi September kati ya lengo la kukusanya shilingi trilioni 1.4 mwezi huo

Kuhusu zoezi la uboreshaji wa taarifa ya namba za utambulisho wa mlipa kodi linaloendelea jijini Dar es Salaam, Bw. Richard Kayombo amesema mpaka sasa TRA imetoa vyeti vipya vya TIN  kwa watu 15, 467 na zimebaki siku tisa kukamilisha zoezi hilo.
 
 Tazama video hapa
 

Waziri Mkuu Akutana na Madudu Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA)

 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amemuagiza Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Bunge), Bw. Uledi Mussa afuatilie malipo ya kiwanja kilichouzwa na CDA kwa sh. milioni 240 lakini fedha iliyoingia ofisini ni sh. milioni 6 tu.

“Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, ninataka ufuatilie mauzo ya kiwanja namba 26 block AA eneo la Kikuyu East ambacho kimeuzwa kwa sh. milioni 240 lakini fedha iliyoingia CDA ni sh. milioni 6 tu. Nataka kujua nani ameingiza milioni 6 na nani kachukua hizo sh. milioni 234,” alisema.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo jana mchana Alhamisi, Oktoba 6, 2016 wakati akizungumza na watumishi na viongozi wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA) kwenye ukumbi wa Hazina ndogo mjini Dodoma.

Bila kutoa ufafanuzi zaidi, Waziri Mkuu alisema eneo hilo lilipaswa kuwa na kituo cha mafuta na akataka apatiwe taarifa mapema iwezekanavyo.

Pia alimwagiza Katibu Mkuu huyo afuatilie mkataba wa upangishaji wa jengo la CDA ambalo wamepangishwa taasisi ya Tunakopesha Limited kwa madai kuwa mhusika alipewa bure na sasa anataka kulipangisha tena ili apate cha juu.

Waziri Mkuu aliwaonya watumishi hao pamoja na viongozi wao waache tabia ya kushirikiana na madalali kuuza viwanja na akawataka wachape kazi wakijielekeza na kasi ya Serikali ya kuhamia Dodoma.

“Tabia ya watumishi kushirikiana na madalali kuuza ardhi sasa basi. Hata hivyo, nimefarijika kukuta mmeanza kuweka mfumo wa kielektoniki katika baadhi ya huduma. Ni lazima mauzo ya viwanja sasa hivi yafanyike kwa njia ya kieletroniki, madalali hawana nafasi,” alisisitiza.

Aliutaka uongozi wa CDA uongeze kasi ya upimaji viwanja kwa sababu mahitaji ni makubwa lakini akaonya kuwa wakati zoezi hilo likifanyika, wananchi walionunua viwanja na bado hawajamalizia kuvilipia, wasinyang’anywe kwa kigezo cha kutaka kuwauzia wengine.

“Mimi nataka idadi ya viwanja vilivyopimwa iongezeke. Lakini pia msitumie fursa hii kuwanyang’anya watu wenye umiliki halali eti kwa sababu Serikali inataka idadi ya viwanja vilivyopimwa iongezeke,” alisema.

“Kama mtu amepewa offer au hati yake asinyang’anywe hata kama amelipia nusu asinyang’anywe. Ahimizwe kumalizia hilo deni na ninyi kazi yenu ni kupima viwanja vingine,” alisisitiza.

“Natambua mnayo benki ya viwanja, lakini inabidi muongeze idadi ya viwanja vingi zaidi. Tumeita wawekezaji waje kujenga nyumba za kuishi watumishi, mahoteli na viwanda na maeneo yote haya inabidi yatengwe rasmi,” alisema.

Alisema jumla ya viwanja 70,000 vimepimwa tangu CDA ianzishwe mwaka 1973. Amesema kama wataendelea na kasi hiyo wakati mahitaji yameongezeka, itawachukua zaidi ya miaka 40 kukamilisha mahitaji ya viwanja 100,000 ambavyo vinatarajiwa kuanza kupimwa hivi karibuni.

Mapema, akitoa taarifa mbele ya Waziri Mkuu, Mkurugenzi Mkuu wa CDA, Eng. Paskasi Muragili alisema usanifu wa upimaji viwanja 20,000 umekamilika na kwamba wana lengo la kupima viwanja vingine 100,000 ifikapo Juni 2017.

Waziri Mkuu alitembelea Ofisi ya CDA na kukagua mfumo wa utunzaji mafaili wa zamani pamoja na uhamishaji wa taarifa za wenye viwanja kwenye mfumo wa kompyuta. Pia alikagua mifumo ya uuzaji viwanja kwa njia ya mtandao ambayo hata hivyo bado haijakamilika.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu alipokea mchango wa zaidi ya sh. milioni moja kutoka kwa Mkuu wa Wilaya wa Kongwa, Bw. Deogratius Ndejembi zikiwa ni kwa ajili ya wakazi wa mkoa wa Kagera walioathirika kwa tetemeko la ardhi lilitokea Septemba 10, mwaka huu.

Pia Waziri Mkuu alipokea mchango mwingine wa zaidi ya sh. milioni tano kutoka kwa makundi mbalimbali ya wafanyabiasha wa Manispaa ya Dodoma wakiwemo wamiliki wa hoteli, nyumba za kulala wageni, waendesha bodaboda na madereva wa daladala.

Akipokea msaada huo, Waziri Mkuu aliwashukuru wafanyabiashara hao na kuwahakikishia kwamba fedha hizo zitapelekwa mkoani Kagera na kuwafikia walengwa kama ilivyokusudiwa.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU

Zitto Kabwe Awamwagia Sifa UKAWA ......Atia Neno Kuhusu Mgogoro wa CUF


Kiongozi Mkuu wa Chama Cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe ameisifia nguvu ya vyama vya siasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kwa kile walichokifanya hasa katika uchaguzi wa mwaka jana.
 
Akizungumza jana katika mahojiano maalum na kituo cha runinga cha Clouds TV, Zitto alisema kuwa chama chake hakiwezi kubeza nguvu kubwa iliyooneshwa na umoja huo na kwamba uliweka historia katika chaguzi zote zilizowahi kufanyika nchini.
 
“Ukawa umeweka historia Kubwa zaidi katika chaguzi za nchi yetu japo kuwa kuna madhaifu ila hatuwezi kupuuza nguvu ile,” alisema Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Mjini.
 
Hata hivyo, pamoja na kusifu nguvu ya muungano huo wa hivyo vya siasa ambavyo ni Chadema, Chama Cha Wananchi (CUF), NCCR-Mageuzi na NLD, Zitto alisisitiza kuwa chama chake hakitajiunga na umoja huo kutokana na maazimio na miiko waliyoiweka katika Azimio la Tabora la chama chake.
 
“Hatukuweza kujiunga na Ukawa kwasababu tuliweka kanuni zetu wazi  tulizozitangaza katika azimio la Tabora,” Zitto anakaririwa.
 
Katika hatua nyingine, Zitto alizungumzia mgogoro wa uenyekiti wa CUF unaoendelea ndani ya chama hicho na kutoa rai kwa vyama vingine vya siasa kutowafarakanisha.
 
Alisema kuwa CUF inapaswa kuachiwa suala hilo walimalize wenyewe katika vikao vyao vya ndani ya chama na sio vinginevyo. 

Aliongeza kuwa kutokana na mgogoro unaoendelea ndani ya CUF, hivi sasa ajenda yao kubwa [kupinga kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi mkuu wa Oktoba]imewekwa kando bali sasa wanatafuta uhalali wa kiongozi wa chama hicho.
 
“Rai yangu tusichochee kabisa mgogoro huu bali ni tuwe kama madaraja ya kufanikisha mgogoro huu kumalizimika kwa amani,” alisema.
 
Hata hivyo, mapema wiki hii Baraza Kuu la Uongozi wa CUF lilifungua shauri mahakamani kuhusu mgogoro wa uongozi ndani ya chama hicho, wakimshataki Msajili vya Vyama vya Siasa nchini pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 Katika shauri hilo, wanapinga uamuzi wa Msajili kuandika barua ya kumtambua Profesa Ibrahim Lipumba kuwa Mwenyekiti halali wa chama hicho huku wakidai kuwa alijiuzulu na taarifa za kujiuzulu kwake waliziwasilisha kwa Msajili.
 
Baraza hilo limedai katika shauri hilo kuwa katiba na sheria ya vyama vya siasa haimpi mamlaka Msajili kuingilia maamuzi ya ndani ya vyama vya siasa. Shauri hilo bado halijaanza kusikilizwa.

Rais Magufuli Atangaza Kiama ....Ni cha Kuwanyang'anya Watu Wote Walioshindwa Kuendeleza Mashamba, Asisitiza Hatojali Hadhi ya Mtu

 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli amewataka watu wote nchini wanaohodhi mashamba makubwa na kutoyaendeleza wafanye hivyo ndani ya mwezi mmoja kabla hayawanyang’aya mashamba hayo kwa mujibu wa sheria na mamlaka aliyonayo.

Akizungumza jana na wananchi mkoani Pwani wakati wa zoezi la kuzindua kiwanda cha kusindika matunda, Rais Dkt. Magufuli alitumia fursa hiyo kuwataka wawekezaji wanaotaka kuja nchini kuwekeza wafanye hivyo kwa kuwa ardhi ipo ya kutosha.

“Nataka watu wote wanaotaka kuja nchini kuwekeza waje, kwa kuwa ardhi ya kutosha tunayo na nawataka watu wote waliohodhi ardhi hata kama walikuwa viongozi huko nyuma nataka wayalime ndani ya mwezi mmoja na kama wasipofanya hivyo nitabatilisha hati zao za umiliki na kuwapa watu wengine ambao wapo tayari kuendeleza ardhi hiyo" Alisema Rais Dkt. John Magufuli.

Aidha Rais Magufuli alisema baadhi ya wafanyabiashara wa sukari nchini wamekuwa siyo waaminifu kwa kuagiza sukari kwa ajili ya matumizi ya viwandani kutoka nje ya nchi sukari ambayo ikifika nchini huiweka kwenye mifuko na kuiuza kwa matumizi ya kawaida ya nyumbani jambo linaloweza kuathiri afya za watumiaji.

“Tatizo la sukari liliingia baada ya kuanza kuifuatilia sukari ili sukari inayopakiwa kwa matumizi ya binadamu iwe hivyo ndipo wafanyabiashara wakaanza kuficha sukari, ndiyo maana ninataka wawekezaji waje hapa kuwekeza katika kilimo cha sukari ili sukari izalishwe hapa nchini” Alisema Rais Dkt. Magufuli.

Pamoja na hayo Rais Magufuli alikemea tabia ya watu kuficha pesa na wengine kuzigeuza katika mfumo wa dolla na kuzificha chini ya ardhi na kusisitiza wanaofanya hivyo mwisho wake watakuta pesa hizo zimeharibika huku akiwataka wazitumie kuwekeza katika viwanda.

Serikali Yachachamaa....Walimu Waliomfanyia Ukatili Mwanafunzi Watimuliwa Chuoni, Mkuu wa Shule Apoteza Kibarua

 
Walimu  wanne wa Chuo Kikuu cha Elimu Dar es Salaam (Duce) na cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere waliohusika kumpiga vibaya mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Mbeya wamefukuzwa chuo huku Jeshi la Polisi mkoani Mbeya likiwashikilia kwa mahojiano walimu wengine watano wa shule hiyo kutokana na tukio hilo.

Aidha, serikali imemvua madaraka Mkuu wa shule hiyo, Magreth Haule kwa kutochukua hatua baada ya kitendo hicho kufanyika shuleni hapo Septemba 28, mwaka huu.

Hatua hizo zimechukuliwa baada ya jana katika mitandao ya kijamii kusambaa kipande cha video kikionesha walimu zaidi ya watatu wakiwa eneo la ofisi wakimshambulia kwa kumpiga makofi, mateke na fimbo sehemu mbalimbali za mwili hasa kichwani mwanafunzi Sebastian Chinguku.

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako ametangaza kuwafukuza chuo walimu wanafunzi hao walioshiriki kitendo cha kumpiga mwanafunzi huyo wa kidato cha tatu wa Shule ya kutwa ya Sekondari ya Mbeya.

Walimu hao ni Frank Msigwa (anayedaiwa kumpiga zaidi mwanafunzi huyo kwa makofi kichwani), John Deo na Sante Gwamaka wote wa Duce na Evans Sanga wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere.

Akizungumza na vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana, Profesa Ndalichako alisema kitendo hicho ni cha kikatili, jinai na kuwa walimu hao wanafunzi hawafai kuendelea na taaluma hiyo ya ualimu na kuwa hatua zaidi za kisheria zinaendelea kuchukuliwa dhidi yao.

Profesa Ndalichako alisema kwa mujibu wa taratibu za vyuo vikuu kitendo kilichofanywa na walimu wanafunzi hao ni kosa la jinai na kuwa hakiwezi kufumbiwa macho.

Alitoa onyo kali kwa wanafunzi wanaokwenda kwenye mafunzo kwa vitendo na kwenda kinyume cha taaluma yao kuwa wanapoteza sifa hivyo amewataka kuzingatia maadili ya fani na taaluma wanazosomea.

Mkoani Mbeya, Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Dhahiri Kidavashari alisema wanawashikilia walimu wa shule hiyo watano kwa mahojiano kuhusu tukio hilo. Hata hivyo, alisema si kwamba walimu hao wanaohojiwa ndio waliohusika na tukio hilo bali wameanza na wale waliopo ili kupata taarifa zaidi.

“Hatuwezi kusema sasa hivi kama wale walimu ndio walioonekana katika kipande cha video kinachosambaa mitandaoni kwa kuwa hili ni suala la mahojiano, tunaamini hawa tulionao wanaweza wakatupa mwanga,” alisema.

Akieleza sababu ya adhabu hiyo, Kamanda alisema katika mahojiano ya awali imebainika kuwa mwalimu wa Kiingereza alitoa kazi, lakini baadhi ya wanafunzi hawakufanya baadaye mwalimu huyo aliwapa adhabu ya kupiga magoti, lakini mwanafunzi huyo alionekana kupinga kwa kueleza ana tatizo la goti hatoweza kufanya adhabu hiyo na mwalimu aliamua kumpeleka ofisini na kumpiga kwa kumchangia.

“Mwalimu aliwaadhibu wanafunzi darasani na alipotaka kumuadhibu mwanafunzi huyo mbele ya darasa, alionesha kupinga kupigwa mbele ya wanafunzi wenzake ndipo alipoamua kumpeleka ofisini na kutokea tukio linalosambaa,” aliongeza Kidavashari.

Katika taarifa yake, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba, alisema Septemba 28 mwaka huu, mwanafunzi Chinguku wa kidato cha tatu wa Shule ya Sekondari Mbeya, mkazi wa Uyole, alipigwa na walimu watatu.

“Nimeelekeza vyombo vya dola Dar es Salaam wawatafute chuoni kwao hao walimu kuhusiana na shambulio hilo kwa mwanafunzi huyo,” ilisema Mwigulu.

Naye Waziri katika Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene ameagiza mamlaka za nidhamu kumvua madaraka Mkuu wa Shule hiyo, Haule kwa kushindwa kuchukua hatua na kutoa taarifa mara baada ya tukio hilo kufanywa na walimu hao shuleni hapo.

"Kwa kuwa waliotenda kosa hili wametoweka tangu Septemba 29, 2016 na hawajulikani walipo, nimesikitishwa kwa kitendo cha mwalimu mkuu wa shule hiyo, Magreth Haule kutochukua hatua. Hii inaonesha kulikuwa na dalili za kutaka kulificha tukio hili baya.

“Na kwa sababu hiyo, pamoja na kwamba wanaendelea kuhojiwa na Polisi, naagiza mamlaka yake ya nidhamu kumvua madaraka mkuu huyo wa shule," alisema Simbachawene katika taarifa yake kwa umma jana.
 Katika hatua nyingine, Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Gratian Mukoba amelaani kitendo kilichofanywa na walimu hao na kukieleza kuwa ni cha mwituni na cha kinyama kwa kuwa hakuna adhabu kama hiyo katika utumishi wa ualimu.

"Nami nimeona hiyo video katika mitandao ya kijamii, kuna sheria za adhabu za viboko lakini si hii walioifanya hao walimu vijana maana walikuwa wakipiga makofi, ngumi, mateke, ngwara. Hizi hazipo kwenye ualimu, lazima wafuate sheria zinazosimamia utumishi wa walimu," alisema Mukoba.

Alishauri vyuo vya ualimu viweke mkazo katika kufundisha walimu vijana namna ya kuwa zaidi ya walimu, kuwa na uvumilivu, subira na kuzingatia sheria. Wafunzwe kisaikolojia kukubali kuwa hawaishii kuwa walimu bali wanaingia kwenye kundi la malezi.

Alisema kwa tukio hilo, ni lazima sheria ichukue mkondo wake ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia hizo hasa walimu vijana kwa kuwa kitaaluma ni tukio la kinyama lisilokubalika.

“Hata kama mwanafunzi ana makosa, amevuta bangi, huwezi kumuadhibu vile, maana pale hujui nani kavuta bangi nani mzima,” alisema Mukoba.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla alisema serikali inalifuatilia kwa karibu tukio la kupigwa kama mwizi mwanafunzi huyo wa shule hiyo ya jijini Mbeya na kusema tayari baadhi ya walimu akiwemo mkuu wa shule, wanashikiliwa na Polisi.

Makalla alibainisha hayo jana kwenye Maadhimisho ya Siku ya Fimbo Nyeupe Duniani yaliyofanyika kitaifa mkoani Mbeya na kusisitiza kuwa walimu waliohusika na tukio la kumpiga mwanafunzi wao kama mwizi wanasakwa na lazima watapatikana.

Alisema Septemba 26, mwaka huu, mwalimu aliyekuwa katika mafunzo kwa vitendo katika shule ya Sekondari ya Mbeya Day aliyemtaja kwa jina la Frank Msigwa alitoa kazi kwa wanafunzi darasani na Septemba 28 alipokuwa akisahihisha kazi zilizofanyika alibaini baadhi ya wanafunzi hawakufanya.

Makalla alifafanua kuwa miongoni mwa wanafunzi aliobaini hawakufanya kazi yake ni pamoja na Chinguku na ndipo aliwatoa nje ya darasa na kuwapa adhabu ya kupiga 'push up' lakini mwanafunzi huyo akagoma akidai kuwa na matatizo ya kiafya katika mbavu zake.

Alisema baada ya kugomea adhabu hiyo mwalimu aliwaamuru wapige magoti lakini pia mwanafunzi huyo aligoma akisema ana matatizo ya goti katika moja ya miguu yake ndipo mwalimu alilazimika kutoa adhabu ya kuwachapa viboko viwili kila mmoja na aliwapiga wote isipokuwa Chunguku ambaye kama alivyofanya kwenye adhabu za kwanza hii pia alikataa.

Alisema baada ya hapo mwalimu huyo alilazimika kwenda kuwaita wenzake wawili ambao nao walikuwa kwenye mafunzo ya ualimu kwa vitendo shuleni hapo na wakambeba mwanafunzi huyo hadi ofisini kwao ambako huko ndiko walianza kumchapa kwa kumchangia kama inavyooneshwa kwenye kipande cha video kilichosambazwa kwenye mitandao ya kijamii.

Kwa mujibu wa Makalla, walimu waliotenda kitendo hicho walitoroka na hawajulikani walipo. Alisema serikali inaendelea kuwasaka huku walimu wengine wakihojiwa Polisi.
 
Click hapa kuona video
 

Thursday, October 6, 2016

Tuesday, October 4, 2016

Polisi Aliyerekodiwa Akipokea Rushwa Kuchukuliwa Hatua

 
Jeshi  la Polisi visiwani Zanzibar, limesema litamchukulia hatua za kinidhamu ofisa wake mwenyewe cheo cha Sajenti ambaye alionekana hivi karibuni akipokea rushwa kutoka kwa raia wa kigeni.

Hatua hiyo, imekuja baada ya picha za video kusambaa katika mitandao ya kijamii, zinazomwonyesha askari huyo akipokea fedha ambazo hadi sasa hazijajulikana kiwango chake kutoka kwa raia huyo wa kigeni, ambaye alikuwa na kosa la kutofunga mkanda.

Katika video hiyo, raia huyo anaokana kutoa fedha na kumkabidhi askari huyo huku akiahidi kumsaidia ili asikamatwe mbele ya safari.

Tukio hilo lilitokea eneo la Mkokotoni Mkoa wa Kaskazini Unguja, ingawa askari huyo alitaja eneo la Mahonda akionyesha nia ovu ya kutenda kosa hilo bila kujijua kama anachukuliwa video.

Kamishna wa Jeshi la Polisi Zanzibar, Hamdani Omar Makame alisema jeshi hilo linampongeza raia huyo wa kigeni kwa kutoa taarifa hiyo.

“Jeshi la polisi linachukua nafasi hii kulaani kosa hili, licha ya kua ni kosa la jinai linalifedhehesha jeshi na kulitia doa kutokana na dhamana kubwa lililokabidhiwa,” alisema.

Alisema kwa mujibu  wa taratibu za jeshi hilo, tayari limeanza uchunguzi mara moja na kwamba litachukua hatua zinazostahili.

Kutokana na hali hiyo, Kamishina Hamdani amewataka wamiliki wa makampuni ya simu za mikononi kufufua mfumo wa upigaji simu kutumia namba za dharura ambazo ni 111 na 112 ili kuwarahisishia wananchi kutoa taarifa.

Tazama Video ya tukio hapa chini.

Wananchi Walioua Watafiti Wakimbia Kijiji Wakihofia kukamatwa na Jeshi la Polisi........Miili Ya Marehemu Yaagwa Jijini Arusha

Baada  ya baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Iringa Mvumi katika  Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma kuwaua watafiti wa Kituo cha Udongo na Maendeleo cha Selian Arusha, wakazi wa kijiji hicho wamehama makazi yao wakihofia kukamatwa na Jeshi la Polisi.

Waandishi wa habari waliofika kijijini hapo jana na walishuhudia hali ya utulivu kijijini hapo tofauti na ilivyozoeleka.

Pamoja na wananchi hao kukimbia makazi yao, taarifa zinasema viongozi wote wa Serikali ya Kijiji hicho  wamekamatwa na polisi wakiwamo Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji, Albert Chimanga na Diwani wa Kata ya Iringa Mvumi, Robert Chikole.

Mmoja wa wakazi wa kijiji hicho aliyejitambulisha kwa jina la Michael Kagisi, alisema kitendo cha wananchi kukimbia kijiji hicho kimesababisha shughuli nyingi za  jamii kusimama   na maduka kufungwa.

Kwa mujibu wa Kagisi, hata wananchi   waliobaki kijijini hapo wakisema    hawakushiriki mauaji hayo, ikifika jioni wanakwenda porini kulala.

“Sehemu kubwa ya watu wameyakimbia makazi yao kwa sababu wanaogopa kukamatwa na polisi, yaani hata shule hazina wanafunzi kwa sababu wengi wamekimbia na wazazi wao.

“Yaani waliouawa waliuawa kwa makosa kwa sababu  kabla ya kuwapiga, walijitetea na kujitambulisha, lakini wananchi hawakutaka kuwasikiliza…   baada ya kuwaua, waliwawekea majani na kuwachoma moto ili wafe haraka,” alisema Kagisi.

Akifafanua, mwananchi huyo alisema siku ya tukio ulikuwapo mkutano kijijini hapo na mwenyekiti wa kijiji alipata taarifa kwamba katika eneo la kutengeneza chumvi, kuna gari ambalo walilitilia shaka kwamba huenda ni majambazi.

“Siku hiyo tulikuwa kwenye mkutano na baadaye tulimuona mwenyekiti akiwaita baadhi ya vijana na kuwaagiza waende eneo la tukio.

“Wale vijana walikwenda huko  walipiga simu kijijini kuwaeleza wananchi, kwamba kuna gari la watu ambao hawaeleweki.

“Taarifa hizo ziliposambaa, wananchi walihamasishana na kuelekea eneo la tukio.

“Walipofika tu, walianza kuwapiga, lakini wale watafiti walijieleza kwamba wao siyo majambazi, huku wakiwaomba wananchi wawapeleke katika ofisi zao za kijiji, lakini wananchi walikataa na kuendelea kuwapiga hadi walipowaua,” alisema.

Naye  Mchungaji wa Kanisa la Biblia kijijini hapo, Donald Nyambuya, alisema kwa sasa maisha kijijini hapo ni ya shida kwa sababu huduma nyingi za  jamii zimefungwa baada ya watu kukimbia makazi yao.

Mwinjilisti wa Kanisa la Waadventista Wasabato (SDA), Jacob Foda, alisema kitendo cha watu kukimbia makazi yao  kimeathiri huduma ya  roho kwa kuwa huwa na kawaida kuwatembelea waumini wake.

Wakati huohuo, simanzi na majonzi, jana, vilitawala wakati wa kuaga miili ya Watafiti wa Kituo cha Utafiti wa Udongo na Maendeleo cha Selian mjini hapa.

Watafiti hao waliuawa juzi na wananchi wa Kijiji cha Iringa Mvumi, wilayani Chamwino, Mkoa wa Dodoma kwa kukatwakatwa mapanga na kuchomwa moto.

Miili hiyo iliwasili mjini hapa jana asubuhi kwa gari ikitokea Dodoma na kuingizwa kwenye eneo la wazi la kituo hicho kilichopo pembeni mwa Uwanja mdogo wa Ndege wa Arusha kwa ajili ya wafanyakazi kutoa heshima za mwisho.

Shughuli ya kuaga miili hiyo ilifanyika asubuhi kwa wafanyakazi, jamaa na marafiki kutoa heshima za mwisho bila majeneza kufunguliwa kwa kuwa imeharibika.

Baadaye  ilipelekwa katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru kwa ajili ya kufanyiwa maandalizi ya kusafirishwa.

Waliouawa katika tukio hilo  walitambuliwa kuwa ni Jaffari Mafuru aliyesafirishwa jana kwenda Mara kwa mazishi, Theresia Ngume, aliyetarajiwa kuzikwa jana mjini Arusha na dereva wa gari walilokuwamo,       STJ 9570 aina ya Toyota Hilux, mali ya Kituo cha Utafiti cha Selian, Nikas Magazine, aliyesafirishwa kwenda Ifakara, Morogoro kwa mazishi.

Watafiti hao  waliuawa wakiwa katika kazi ya mradi unaoandaa taarifa za hali ya udogo kwa nchi nzima.

Akizungumza baada ya kutoa heshima za mwisho, Mkurugenzi wa Kituo hicho, Januari Mafuru ambaye ni baba mzazi wa marehemu Jaffari, alisema tukio hilo limemuumiza sana.

Alisema kituo hicho kimekuwa kikiendesha mradi huo kwa lengo la kuwasilisha taarifa hizo kwa wakulima wadogo na wataalamu wa kilimo  ziweze kuwasaidia wananchi katika kilimo na hatimaye kuongeza mazao.

“Mradi huu umemaliza utafiti katika Mikoa ya Kanda ya Kaskazini ya Kilimanjaro, Arusha na Manyara. Baada ya hapo kazi nyingine ilikuwa imeanza Kanda ya Kati Dodoma na Singida.

“Wiki iliyopita, tuliandaa watafiti wanane na magari yao manne kwa ajili ya kwenda mkoani Dodoma kukusanya udongo kwa ajili ya kuuleta hapa kwenye maabara za Seliani kufanyiwa utafiti kisha kutoa matokeo yatakayowarudia wakulima,” alisema Mafuru.

Akizungumzia kuwasili kwa watafiti hao katika Kijiji cha Iringa Mvumi, wilayani Chamwino yalikotokea mauaji hayo, Mafuru alisema timu zote zilikuwa na barua za utambulisho pamoja na vifaa vya kazi.

“Timu iliyokuwa Chamwino katika Kijiji cha Iringa Mvumi, iliwakuta wanawake wakiendelea na shughuli za kukusanya chumvi  na watafiti waliwasilimia na kujitambulisha wametokea wapi.

“Taarifa tulizonazo ni kwamba, baada ya kusalimia, watafiti waliacha gari pembeni na kutembelea maeneo   kuchagua udogo.

“Huku nyuma kundi la wale wanawake lilitoa taarifa kwa viongozi wao kuwa wamevamiwa na wanyonya damu, ndipo walipotokea watu wakiwa na mashoka na mapanga na   kuwashambulia kabla ya kuwachoma moto,” alisema.

Mtafiti Mwandamizi wa Kituo cha Selian, Dk. Lameck Makoye, alilaani mauaji hayo na kusema hajawahi kuona wala kusikia watafiti wakivamiwa   wanapokuwa   vijijini.

“Naamini Serikali imeona, binafsi sijawahi kuona tukio la aina hii kwa sababu  watafiti wale walikuwa na vielelezo vyote vinavyowatambulisha.

“Hata mradi waliokwenda kufanya ulikuwa ni kwa faida ya wananchi wa Kijiji cha Iringa Mvumi kwa vile umelenga maeneo ya nchi nzima.

“Sisi Kituo cha Utafiti cha Selian ndiyo tunaoleta maendeleo ya mkulima kwa nchi nzima kwa kufanya utafiti wa udongo unaomwezesha mkulima alime vipi na atumie mbolea kwa kiwango gani na ya aina gani,” alisema Dk. Makoye.

Mume wa marehemu Theresia, Jonas Mjema, akizungumza kwa huzuni kuhusu  kuondokewa na mkewe, alisema kabla ya tukio la mkewe kuchomwa moto, alizungumza naye asubuhi kujua anaendeleaje.

“Niliwasiliana naye asubuhi Jumamosi tukatakiana kazi njema, ilipofika jioni nilimtafuta lakini simu yake haikupatikana.

“Nilijipa matumaini labda mawasiliano hayakuwa mazuri kwa vile shughuli zao ni za porini.

“Ilipofika Jumapili, nilipigiwa simu na shemeji yangu akinipa taarifa za tukio la kuchomwa moto mke wangu,” alisema Mjema aliyeachwa na watoto wawili.

Aliyetoa taarifa za maiti kufufuka ikiwa mochwari Singida ashikiliwa na Polisi

Jeshi la polisi mkoa wa Singida, linamshikilia askari mgambo mwajiriwa hospitali ya mkoa, MG 7822 Emmanuel Daghau (42) kwa tuhuma ya kutoa taarifa za uongo juu ya maiti kufufuka ikiwa kwenye chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali ya mkoa.

Imedaiwa kuwa uongo huo ulizua mtafaruku mkubwa kwa ndugu na jamaa wa merehemu Rahel Erasto (28), aliyekuwa mkazi wa Minga manispaa ya Singida.

Kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Singida, SSP Mayala Towo, alisema tukio hilo limetokea Septemba, 30 mwaka huu, majira ya alasiri huko katika hospitali ya mkoa mjini hapa.

Akifafanua, kaimu kamanda huyo alisema kuwa Septemba, 29 mwaka huu Rahel (marehemu) alifikishwa katika hospitali hiyo ya mkoa, kwa ajili ya kupata huduma za kujifungua salama.

“Kutokana na sababu za kitabibu Rahel, alishindwa kujifungua kwa njia ya kawaida na hivyo ililazimika kufanyiwa upasuaji ambapo mtoto wa kiume alitolewa akiwa hai, Lakini mama kwa bahati mbaya alifariki dunia usiku saa saba Septemba, 30. Mimba hiyo ilikuwa ya kwanza kwa marehemu Rahel,” alisema kaimu kamanda huyo.

Akifafanua zaidi, alisema kuwa baada ya Rahel kufariki dunia, mwili wake ulipelekwa mochwari ambapo kesho yake, ndugu walijikusanya eneo hilo wakijadiliana namna kuuchukua mwili kwa ajili ya kwenda kuzika.

Alisema kuwa wakati ndugu wakiendelea kuzungumzia masuala ya mazishi, alijitokeza mlinzi Daghau na kuwaeleza kuwa ndugu yao huyo, alifariki kutokana na uzembe na kwamba usiku akiwa kwenye doria za kawaida, alisikia marehemu akipiga chafya na aliposogelea dirishani, alimwona akiwa amefufuka.

Towo alisema kuwa awali mgambo huyo baada ya kuhojiwa na Polisi, alikiri kumwona marehemu huyo akiwa amefufuka na alisikia akipiga chafya. Alikiri kwa maandishi na kuweka saini yake.

Alisema lakini baada ya Emmanuel kubaini kuwa baadhi ya ndugu wa marehemu na watoa huduma za afya hospitali ya mkoa kudai kuwa Rahel amefariki dunia kutokana na matatizo ya kawaida ya uzazi na wala hakufa na kufufuka, alipohojiwa mara ya pili, alikana maelezo yake ya awali aliyotoa kwa Polisi.

Wifi wa marehemu Rahel, Mary Mpaki, alikiri kuwa alimsikia mlinzi Emmanuel wakati akiwatangazia waombolezaji kuwa marehemu amefariki dunia kutoka na uzembe wa madaktari, na kwamba alipelekwa chumba cha kuhifadhia maiti akiwa hai.

“Kama ndugu wa marehemu ambao baada ya kufanyiwa upasuaji kuna ndugu ambao walitaka kulala wodini lakini hawakuruhusiwa.Tuliposikia maneno ya mlinzi huyo, tuliamini kwa asilimia mia moja maneno yake kwamba Rahel alipelekwa mochwari akiwa bado yu hai,” alisema kwa masikitiko.

Mary alisema baada ya taarifa ya mlinzi huyo, walienda moja kwa moja kituo cha Polisi kutoa taarifa hizo za kusikitisha.

Ndugu wa marehemu ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema taarifa iliyotolewa na mlinzi kuwa Rahel alifufuka na kupiga chafya, zitakuwa ni za ukweli kwa sababu Ni mtu mwenye akili, hawezi kudanganya jambo hilo.

“Tunasikia kwamba mlinzi kala matapishi yake kwa kitendo cha kukanusha taarifa alizotoa awali kituo cha Polisi. Kama amefanya hivyo, itakuwa kuna shinikizo amepata hivyo anatafuta njia ya kujiokoa,” alisema.

Kaimu mganga mkuu wa mkoa, Dk.Ramadhani Kabala, alikiri kuwepo kwa taarifa hizo na kudai kwa sasa mwili wa marehemu unaendelea kufanyiwa uchunguzi, ili kutambua kama kweli Rahel alifufuka na kupiga chafya akiwa ndani ya chumba cha kuhifadhia maiti.

“Ingawa si rahisi binadamu kufufuka baada ya kufariki dunia, lakini hatuwezi kuzipuuza taarifa hizi za mlinzi. Ipo timu inaongozwa na daktari bingwa kutoka wiraza ya mambo ya ndani, Dk.Ahmed Makata inaendelea na uchunguzi wa kina. Kwa hiyo baada ya kumalizika kwa uchunguzi, tutawaita waandishi wa habari kuwaeleza ukweli ili muweze kuitaarifu jamii,” alisema Dk.Kabala.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Singida, Mhandisi Mathew Mtigumwe, alikiri kupokea taarifa hiyo ya aina yake, na kwamba zipo timu mbili zinaendelea na kuchunguzi ili ukweli uweze kubainika.

Na Nathaniel Limu, Singida

UPDATED!: List Ya Vyuo Vilivyotoa Selection Ya Majina Ya Wanafunzi Waliochaguliwa Vyuo Vikuu Mbalimbali 2016/2017


Kuona Majina Ya Wanafunzi Waliochaguliwa Chuo Kikuu 2016/2017,
 
 ==>Chuo Kikuu Arusha    <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Cha Mipango Dodoma   <<bonyeza Hapa>>


==> Sokoine University- SUA   <<Bofya Hapa>>

==>Chuo Kikuu Suza-zanzbar  <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Kikuu Saut-mbeya      <<bonyeza Hapa>>


==>Chuo Kikuu Saut-arusha     <<bonyeza Hapa>>
 
==>Chuo Cha MUM-Morogoro(2nd Round)   <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Cha Ushirika-moshi MUCCOBS(MoCU)   <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Cha Maji-ubungo    <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Cha Tumaini- Dar  << bonyeza Hapa>>

==>Chuo Kikuu Ardhi    <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Kikuu Sekomu     <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Cha Mweka-moshi      <<bonyeza Hapa>>

 ==> 
Chuo Kikuu St. John's Dodoma    <<Bonyeza  Hapa>>

==> Chuo cha Tax Management- ITA  <<Bonyeza Hapa>>

==> Chuo Kikuu Huria -OUT  <<Bonyeza Hapa>>
 
==> TEKU     <<Bonyeza Hapa>>
 
 ==>Chuo Kikuu Ruaha    <<Bonyeza Hapa>>
 
==> Chuo Kikuu Iringa    << Bonyeza Hapa>>
 
==> Chuo kikuu Bugando  <<Bonyeza Hapa>>
 
==>Chuo  Kikuu Cha Mwalimu Nyerere   <<bonyeza Hapa>> 

==>Chuo  Kikuu Cha  Udsm,duce Na Muce   <<bonyeza Hapa>> 

==>Chuo  Kikuu Cha  Tumaini Makumira    <<Bonyeza Hapa>>   

==>Chuo  Kikuu Cha Udom  <<bonyeza Hapa>>

 ==>Chuo  Kikuu Cha Ifm <<bonyeza Hapa>>

==>Chuo Kikuu Marian << Bonyeza Hapa>>

 ==>Chuo Kikuu Cbe        << Bonyeza Hapa>>

==>Tumaini-mbeya     << Bonyeza Hapa>> & <<hapa>>

 ==>Chuo Kikuu Mum         << Bonyeza Hapa>>

==>Chuo Mum(Diploma) <<Bonyeza Hapa>>

 ==>Chuo- Stella Maris   << Bonyeza Hapa>>

 ==>Chuo- Kampala-kiu  << Bonyeza Hapa>>